Na Mwandishi Wetu
RAIS Jakaya Kikwete amealikwa kuhudhuria sherehe za kuapishwa kwa Rais Joseph Kabange Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo zikazofanyika Desemba 6, mwaka huu mjini Kinshasa.
Mwaliko huo uliwasilishwa kwa Rais Kikwete juzi jioni Ikulu jijini Dar es Salaam na mjumbe maalum wa Kabila, Vital Kamerhe.
Akipokea mwaliko huo, Kikwete alimpongeza Kabila kwa kufanikisha uchaguzi mkuu wa kwanza nchi humo kwa zaidi ya miaka 40 sasa na kuchaguliwa kuwa rais.
Akizungumza baada ya kupokea mwaliko huo, Rais Kikwete amewashauri raia wa nchi hiyo kuanza kazi ya kujenga nchi yao ambayo ni tajiri sana barani Afrika
"Kikubwa kwenu ni kuanza kazi ya kujenga nchi, lazima watu waone tofauti, kongo sio nchi maskini," alisema na kusisitiza haja ya kuweka miundo mbinu, huduma za jamii kama hospitali na shule ili watu waanze kuishi maisha kamili na kukuza amani.
Vilevile ameahidi kushirikiana na nchi hiyo na kueleza azma yake ya kutaka kushirikiana kujenga miundo mbinu imara, itakayokuza na kuimarisha biashara na uchumi kati ya nchi hizo ikiwamo reli, barabara, bandari na kuimarisha biashara katika ukanda wa nchi za maziwa makuu.
Awali mjumbe huyo wa Kabila alimweleza Rais Kikwete kwamba Mahakama Kuu nchi humo, inatarajiwa kutoa uamuzi wa pingamizi liliowekwa na mpinzani wa Rais Kabila katika uchaguzi huo, Jean-Pierre Bemba kuanzia leo.
Mapema akiwa katika Ikulu ya Zanzibar, Rais Kikwete alipokea mwaliko kutoka kwa Rais Jacques Chirac wa Ufaransa akimtaka kuhudhuria mkutano wa wakuu wa nchi kati ya Ufaransa na Afrika, utakaofanyika Februari mwakani nchini humo.
Mwaliko huo, uliwashilishwa asubuhi na Waziri wa Ushirikiano na Maendeleo wa Ufaransa, Brigitte Girardin.
Kikwete alikubali mwaliko huo na kuishukuru nchi hiyo kwa misaada yake kwa Tanzania kufuatia makubaliano yaliyotiwa saini ya kuendeleza huduma za afya, elimu, maji na utalii kwa kipindi cha miaka mitano ijayo. Kiasi cha Sh70 bilioni za kitanzania zitatumika katika kuendeleza miradi hiyo.
Rais alitumia fursa hiyo kuiomba Ufaransa isaidie Tanzania kupata kocha wa timu vijana wadogo kwa lengo la kuwalea na kuwafundisha ili baadaye ije kuwa na timu kamili yenye ujuzi.
Awali Rais Kikwete alikutana na ujumbe wa wafanyibiashara kutoka Kuwait ambao wamekuja nchini kuitikia wito wake wa kutafuta maeneo ya uwekezaji.
Wafanyabiashara hao ni Mkurugenzi na Mwenyekiti wa Mamlaka ya Bandari Kuwait, Fadhel Ali Baghli na Waziri wa zamani wa viwanda na Biashara wa nchi hiyo, Dk Yousef Al Zalzalah.