Na Muhibu Said
MAFUNZO ya fani mbalimbali yanayotolewa na Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) cha jijini Dar es Salaam yataanza kutolewa kwa njia ya mtandao wa kompyuta ili kuwasaidia wanafunzi walioko mikoani.
Utaratibu huo mpya ambao unaendelea kuandaliwa na chuo hicho, unalenga kukidhi mahitaji ya mafunzo ya fani hizo kwa watu wengi zaidi kwa gharama nafuu.
Mkuu wa chuo hicho, Profesa Joshua Doriye alisema alipokuwa akihutubia katika mahafali ya 32 ya chuo hicho, yaliyofanyika chuoni hapo Ijumaa.
Alisema chuo bado kinaendelea na utafiti wa kuona uwezekano wa kufundisha fani hizo kwa njia ya mtandao wa kompyuta mikoani.
Alizitaja fani zinazofundishwa na IFM kuwa ni, benki, bima, hifadhi ya jamii, uhasibu, kodi, sayansi ya kompyuta, teknolojia ya habari na usimamizi wa Fedha.
Naye Naibu Waziri wa Fedha, Mustapha Mkullo, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mahafali hayo, alisema uamuzi wa kukifanya chuo hicho kuwa chuo Kikuu kama ilivyoombwa na uongozi wa chuo, utatolewa na serikali mapema ili kuuwezesha kutekeleza mipango yake.
Mkullo, aliahidi pia kuwasilisha kunakohusika maombi ya ufadhili wa ukarabati wa majengo ya chuo na kuboresha elimu, lililotolewa katika mahafali hayo.
Mwenyekiti wa Baraza la Chuo, Profesa Leticia Rutashobya, alisema azma ya kukipa chuo hicho hadhi hiyo, ni miongoni mwa malengo ya Mpango wa Maendeleo ya mwaka 2004/2005 ili kukabiliana na nguvu ya soko la ajira iliyopo ambayo kwa kiasi kikubwa huhitaji kuajiri watu wenye shahada ya Chuo Kikuu.
"Tunaamini kuwa Chuo cha Usimamizi wa Fedha kimejiandaa vema katika mwelekeo wa kutoa shahada katika fani mbalimbali ili kukidhi mahitaji ya soko la ajira na kutoa huduma kwa jamii katika mazingira mapya ya kiuchumi, soko huria na mabadiliko makubwa ya teknolojia," alisema Profesa Rutashobya.
Wahitimu 968 walitunukiwa vyeti katika ngazi za cheti, Stashahada na Stashahada ya Uzamili.