MKURUGENZI wa Chuo cha Uandishi wa Habari na Mawasiliano ya Umma (IJMC), Profesa Mwajabu Posi, ameanza kuonja machungu ya migomo ya wanafunzi vyuoni.
Katika mkutano kati ya uongozi na wanafunzi uliofanyika chuoni hapo jana, Profesa Posi alijitahidi kujenga hoja za kuwaridhisha wanafunzi, lakini bado akawa katika wakati mgumu.
Alijitahidi kutoa ufafanuzi wa fedha zilizotolewa chuoni hapo kwa ajili ya mafunzo ya vitendo, lakini wanafunzi wakawa hawataki kupokea kiasi wanachopewa sasa.
Wanafunzi wa mwaka wa kwanza wanapewa sh 18,000; ilhali wa mwaka wa pili na wa tatu wakipewa sh 30,000 badala ya sh 120,000.
“Leo tumeshapata fedha zenu, ziko tayari tumefanya kama mlivyotutuma, lakini wanafunzi wa mwaka wa kwanza watapata kiwango cha sh 18,000 kwa kuwa hawakuwapo kwenye mapendekezo ya maombi ya vifaa hivyo.
“Ila wa mwaka wa tatu tutawapatia sh 30,000 kwa kuwa ndio waliokuwapo wakati huo,” alisema Profesa Posi.
Wanafunzi hawakufurahishwa na taarifa hiyo, hivyo walianza kupaza sauti.
Mwanafunzi Abdallah Selemani wa mwaka wa tatu, aliendelea kudai maelezo, akitaka kujua sababu za kupewa kiasi kidogo, na kiongozi aliyeamua hivyo.
Mkurugenzi huo aliamua kutoa maelezo zaidi kwa kusema kuwa mapendekezo waliyoyaomba yako kwenye mchakato.
Naye, Makamu Mkuu wa IJMC, Anastazia Rugaba, alisema: “Kwani hakuna binadamu ambaye si mkosaji au msahaulifu?
“Ninaomba tuelezwe kuwa nini kinafanyika, ili kupata ufumbuzi huo ili wanafunzi waendelee na masomo,” alisema.
Mkurungezi huyo baada ya kuona bado wanafunzi hawaridhiki na majibu, alimpa nafasi Mhasibu wa Chuo aliyejulikana kwa jina la Ngoma ili atoe maelezo.
“Tuliamua tuwape fedha hizo kwanza,” alisema Ngoma.
Jibu hilo nalo halikuwaridhisha, ndipo wanafunzi hao walipoomba uongozi wa Bodi ya Mikopo uende chuoni hapo kutoa ufafanuzi.