MGAWO wa umeme nchini utaendelea hadi Agosti, 2007, mamlaka husika imethibitisha.
Ofisa Uhusiano wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Daniel Mshana, amesema ingawa mgawo halisi unakusudiwa kumalizika muda huo, makali yake hayatakuwa kama haya wanayopata wananchi sasa.
Mshana alisema hayo jana asubuhi alipokuwa akizungumza katika kipindi cha ‘Power Breakfast’ kinachorushwa hewani na redio ya Clouds FM, yenye makao yake Dar es Salaam.
Alisema Bwawa la Mtera limefungwa, wakati Bwawa la Nyumba ya Mungu na Bwawa la Kihansi; kina cha maji hakiwezi kuendesha mitambo inayozalisha umeme.
“Hali ya sasa ya upatikanaji umeme nchini imezidi kuwa ngumu kwa sehemu fulani, tunategemea kuwa mgawo huu utaendelea hadi Agosti mwakani, ambako mitambo ya kukodi itakuwa imeanza kuzalisha kwa kiwango kikubwa,” alisema Mshana.
Alisema kwa siku za karibuni, TANESCO inategemea zaidi umeme unaotokana na maji ya Mto Pangani. Unazalisha megawati 68.
Alisema baada ya kina cha maji kushuka katika bwawa hilo, hali ya mgawo imezidi kuwa mbaya, sambamba na kuharibika kwa mtambo wa Kampuni ya Songas.
“Naamini kama tutafanikiwa kujiunga na gridi ya Zambia, tunaweza kupunguza kwa kiasi kikubwa suala hili la mgawo, lakini pia itakuwa njia nzuri kwa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Uchumi ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) katika kupambana na suala hili,” alisema Mshana.
Mji wa Sumbawanga mkoani Rukwa, unapata huduma ya umeme kutoka Zambia.
Kuhusu Kampuni ya Richmond, iliyoingia mkataba wa kuzalisha umeme, Mshana hakuwa tayari kuizungumzia kwa undani, ingawa alikiri kuchelewa kwa kampuni kuanza uzalishaji wa umeme. Mahitaji ya umeme kwa nchi nzima ni megawati 580.