WAZIRI Mkuu, Edward Lowassa, amechukizwa na kitendo cha viongozi wa Manispaa ya Ilala, kushindwa kuchukua uamuzi haraka wa kupiga marufuku kilimo cha mchicha katika Bonde la Msimbazi.
Lowassa, alisema baada ya taarifa ya wataalamu kuonyesha kuwa maji katika bonde hilo hayafai kumwagia mchicha, viongozi hao walipaswa kufanya utaratibu haraka wa kuokoa maisha ya wananchi.
Mbunge wa Viti Maalumu, ambaye pia ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba (CCM), ndiye aliyetoa ‘siri’ ya utafiti wa wataalamu wa maabara.
Waziri Mkuu alielezwa kwamba vipimo vya maabara vimebaini kuwapo kwa vimelea vinavyosababisha ugonjwa wa kipindupindu.
Kutokana na taarifa hiyo, Lowassa aliunga mkono upigaji marufuku biashara ya mchicha kutoka bonde hilo.
Aliiagiza manispaa husika ifanye tathmini ya thamani ya mchicha wa kila mkulima katika bonde hilo, ung’olewe, kisha wahusika walipwe fidia.
Aliagiza kuwa baada ya kuung’oa, wakulima hao watafute maeneo mengine kwa kilimo chao, kwani eneo hilo sasa halifai kwa kilimo hicho kutokana na madhara makubwa ya kipindupindu na magonjwa mengine.
Mkurugenzi wa Manispaa na Kinondoni, Hussein Katanga, alisema manispaa yake ipo tayari kuununua mchicha huo na kuuteketeza.
Mkurungenzi huyo alisema idadi ya wagonjwa wa kipindupindu katika Kambi ya Mburahati ni 28. Ugonjwa huo ulianza Desemba 31. Hadi jana, watu 46 wamekufa.
Naye Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke, Idd Nyundo, akitoa taarifa kwa Waziri Mkuu, alisema takwimu za wagonjwa wa ugonjwa huo hadi jana katika kituo cha Tambuka Reli kulikuwa na wagonjwa 10. Watu wengine 43 wamekufa kwa ugonjwa huo hadi jana.
Katika kambi ya Buguruni kwa Mnyamani, Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, John Lubuva, alisema ugonjwa huo ulianza Desemba 2, mwaka jana hadi jana, wagonjwa 4,913 walilazwa kambini hapo na kupatiwa matibabu. Wagonjwa 24 kati yao walikufa.
Katika hatua nyingine, Lowassa, alikasirika baada ya kuambiwa kwamba wahudumu wa wagonjwa wa kipindupindu, hawajalipwa fedha kwa muda mrefu. Manispaa zilizoshutumiwa ni Kinondoni na Temeke.
Lowassa, alikubaliana na mpango wa mkoa wa kuhakikisha kuwa ugonjwa wa kipindupindu unatokomezwa mkoani Dar es Salaam ndani ya kipindi cha wiki mbili.
“Nimetembelea kambi zote, nimeshangaa kwa nini ugonjwa huu unaendelea kwa kasi ya aina hii tangu mwaka jana, sioni sababu ya kufanya utushindwe, kinachotakiwa ni kujipanga vizuri, na hii ni aibu.
“Jukumu la kuondoa ugonjwa huu liko ndani ya viongozi wote wa manispaa, wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa Abbas Kandoro,” alisema.
Chanzo kikuu cha ugonjwa wa kipindupindu ni uchafu.
Ugonjwa huu unaenezwa kirahisi na nzi, vyakula, matunda na maji yasiyochemshwa na kuhifadhiwa vema.
Dalili za mgonjwa wa kipindupindu ni kuharisha kinyesi chenye rangi inayofanana na maji ya mchele uliooshwa, na kupoteza nguvu.
Inashauriwa kuwa mara dalili hizo zinapoonekana, huduma ya kwanza ni kwa watu walio karibu kukoroga maji yenye sukari nyingi na kumpa mgonjwa. Maji hayo yatamsaidia kumpa nguvu mgonjwa. Mgonjwa lazima apelekwe hospitali haraka ili kuokoa maisha yake.
Ugonjwa huu unaambuza kirahisi, hivyo hata wale wanaohudumia wagonjwa wa aina hiyo, wanapaswa kuwa makini.