Na Alphan Mlacha
WAZIRI wa Viwanda Biashara na Masoko, Bazil Mramba, amesema utegemezi wa nchi zinazoendelea umechangia kwa kiasi kikubwa kwa nchi za Afrika kukosa maendeleo na kuwa na idadi kubwa ya watu wasio na ajira.
Waziri huyo alisema hayo jana jijini Dar es Salaam katika warsha ya siku mbili iliyowahusisha wataalamu mbalimbali wa uchumi na fedha kutoka Ulaya, Asia, Brazili na baadhi ya nchi za Afrika.
Alisema utegemezi uliopo ni wa wataalamu wa nyanja za kilimo na biashara, pamoja utegemezi wa fedha kwa ajili ya kuendesha shughuli mbambali katika nchi zinazoendelea.
Alisema nchi za Afrika zinaweza kujikwamua kiuchumi kwa kuzalisha kwa wingi mazao ya chakula na biashara na kutafuta masoko ndani ya Afrika kabla ya kufikiria masoko ya nje ya bara hilo.
Alisema mfano mzuri ni soko la Afrika Mashariki ambalo kwa sasa lina watu zaidi yamilioni 90 wanaoweza kuwa wateja wazuri wa bidhaa zinazozalishwa katika nchi hizo.
Alifahamisha kuwa ili kukuza soko hilo, ipo haja ya kuboresha miundombinu, kwa ajili ya kuwezesha wanunuzi kufika kwenye maeneo ya uzalishaji kwa urahisi.
Alitoa mfano wa zao la korosho kuwa lina soko kubwa duniani, lakini uzalishaji wake unahitaji kuboreshwa ili kufikia viwango vya soko la kimataifa na kuweza kuhimili ushindani.