Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI Game Stores kutoka Afrika Kusini, inatarajia kuwekeza nchini dola za Marekani 129.6 milioni (zaidi ya Sh130bn) katika sekta ya biashara katika kipindi cha miaka 10 ijayo.
Uwekezaji huo pamoja na mambo mengine utahusu uhifadhi wa bidhaa za viwandani zinazozalishwa nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa Game Stores, Fanus Nothnagel, alisema jijini Dares Salaam jana kwamba, uwekezaji huo kwa Bohari ya Dar es Salaam utazalisha ajira 110.
Mkurugenzi huyo alifafanua kwamba, kati ya ajira hizo 50 zitakuwa za kudumu, 60 za muda maalumu ambazo zitakuwa katika vitengo vya fedha, ulinzi na usafi. Nothnagel alitaja nafasi nyingine za ajira kwamba zitahusu ufundi na mambo ya ushuru.
Alisema gharama za kuhifadhi bidhaa katika bohari hizo zitakuwa za kawaida ambazo zimelenga kuchangia ukuaji wa uchumi wa nchi.
Game Stores imekwishawekeza katika bohari 69 katika nchi nane za bara hili.