Irene Lipende (TSJ) na Alphan Mlacha
WAWEKEZAJI kutoka Falme za Kiarabu, wameitikia wito wa Rais Jakaya Kikwete na kuja nchini kuanzisha benki ili kutoa huduma za fedha na mikopo kwa Watanzania.
Benki inayotarajiwa kuanzishwa itakuwa inaitwa Islamic Bank, ambayo itakuwa na jukumu la kutoa huduma za fedha kwa wananchi wote bila kubagua.
Akizungumza na wawekezaji hao jana, Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji, Dk Juma Ngasongwa, alisema benki hiyo ambayo inatarajia kutoa mikopo mbalimbali, inategemewa kukuza uchumi wa wafanyabiashara.
Naye Kiongozi wa Benki hiyo yenye Makao Makuu yake Kuwait, Anwar Ibrahim, alisema ujio wao unafuatia wito wa Rais Kikwete ambaye aliwaomba kuja kuwekeza Tanzania kutokana na mazingira mazuri ya biashara.
"Ni kweli na tumekubali kuwa mazingira ni mazuri kwa biashara, ni matumaini yetu kuwa tutaweza kufanya biashara vizuri na Watanzania kwani benki zetu zitakuwa zikitoa mikopo nafuu kwa wananchi,’’ alisema Ibrahim.
Ibrahim, aliwaondoa wasiwasi Watanzania kuhusiana na imani zao, kwani benki hiyo itatoa huduma kwa watu wa imani zote.
Alisema tayari benki hiyo imefungua ofisi Kenya ambapo Wakristo ni wengi na ndio wanaotumia benki hiyo kuliko Waislamu.
Dk Ngasongwa, alisema ziara za Rais Kikwete zinategemewa kuzaa matunda zaidi kwani, wawekezaji kutoa China wamekubali kuja nchini kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa umeme kwa kutumia mkaa wa mawe huko Kiwira kutoka megawati sita za sasa hadi 200.
Aliongeza kuwa, pia Korea ya Kusini walikubali kujenga daraja la Mto Malagarasi ambalo linatarajia kugharimu zaidi ya dola za Marekani 25 milioni.
Wakorea pia, wamekubali kusaidia wakulima kuinua kilimo kwa kuanzisha miradi ya umwagiliaji na kwamba, watachimba mabwawa kwa ajili ya umwagiliaji mashamba na uvunaji wa maji ya mvua.
Tayari, Kampuni ya Samsung imekubali kuja nchini kwa ajili ya kuwekeza katika uzalishaji wa umeme wa gesi ya Kinyerezi na kuunda bidhaa zao nchini, ili kukuza soko na ajira kwa Watanzania .
Dk Ngasongwa, alisema Kuwait pia wamekubali kuja kushughulikia suala la uzalishaji wa gesi na mafuta kwa maeneo ya Tanzania ambayo yameonyesha kuwa na nishati hiyo.