Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imetoa kibali cha kutumia nembo ya Taifa kama vile bendera ya Taifa kwenye matangazo ya shughuli pamoja na bidhaa za kibiashara, katika sherehe za kuadhimisha miaka 45 ya uhuru wa Tanganyika.
Taarifa hiyo iliyotolewa jana na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Joseph Mungai, na kusainiwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, inaeleza kibali hicho ni kuanzia Novemba 14 hadi Desemba 31, 2006.
“Matumizi ya nembo ya taifa yatakuwa kwa ajili ya matangazo ya shughuli mbalimbali pamoja na bidhaa za kibiashara zitakazotolewa kwa ajili ya sherehe za kuadhimisha miaka 45 ya uhuru,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Kibali hicho kimetolewa kulingana na kifungu cha 6 (2) ya nembo ya taifa ya mwaka 2002, chenye kumpa mamlaka Waziri wa Mambo ya Ndani kufanya hivyo.
“Kwa mantiki hiyo, kibali hiki cha Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, kimetolewa kwa taasisi mbalimbali na wafanyabiashara kwa dhamira ya kuwashirikisha kikamilifu katika maadhimisho hayo ya kitaifa.”
Tanganyika husherehekea uhuru wake kila Desemba 9 na mwaka huu inasherehea ikiwa ni mwaka wa 45 tangu ilipopata uhuru huo kutoka kwa Waingereza Desemba 9, 1961.