Na Charles Mwakipesile, Mbeya
MKULIMA wa Kijiji cha Utengule Wilaya ya Mbarali, Bw. Zakaria Mfumbulwa, ameuawa kikatili na mfugaji wa kijiji hicho katika mapigano yaliyotokea jana wakati alipokuwa akijaribu kuzuia mifugo kutoingia katika shamba lake.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mmoja wa wajumbe wa Kamati maalumu ya kuwaondoa wafugaji wanaovamia mashamba wilayani humo baada ya kuondolewa katika bonde la ardhi oevu la Ihefu, Bw. Kenneth Ndingo, alisema ugomvi huo ulitokea jana.
Alisema kuwa mfugaji huyo ambaye hadi sasa hajapatikana kutokana na madai kuwa alikuwa kibarua aliyekuwa anafanya kazi ya kuchunga ng'ombe hao , aliipeleka mifugo hiyo katika shamba la Bw. Mfumbulwa.
Bw. Ndingo, alisema kuwa marehemu kuona hali hiyo alizuia kitendo hicho kisifanyike , ndipo ugomvi ulipoanza kwa kupigana kwa kutumia fimbo hali iliyomfanya mfugaji huyo kuchomoa kisu kiunoni na kumchoma mkulima huyo.
Alisema mfugaji huyo alifanya mauaji hayo 'kijanja' mkubwa kwani wakiwa wamekumbatiana alimchoma kisu na kutokana na maumivu makali, alidondoka na kupoteza maisha.
Bw. Ndingo alisema kwa kuwa hapakuwa na mtu wakati wanapigana, mfugaji huyo alitumia mwanya huo kutorokana na hadi sasa hajakamatwa na polisi wanaendelea kumsaka.
Mapigano ya aina hiyo yamekuwa yakifanyika mara kwa mara tangu kuanza kwa maandalizi ya msimu wa kilimo ambapo wafugaji waliondolewa katika hifadhi hiyo, wamekuwa wakivamia mashamba kwa ajili ya kulisha mifugo yao kwa nguvu.
Mara kwa mara vinapofanyika vitendo hivyo, wakulima wamekuwa wakija juu hali inayowafanya wafugaji kutumia silaha zikiwemo fimbo na visu kuwapiga wakulima kwa madai kwamba hawana sehemu za kwenda.
Hata sasa wafugaji wengi wameondoka wilayani humo kwenda katika mikoa ya Lindi na Pwani walikopangiwa na Serikali ambapo wanaoruhusiwa kubaki ni wale wenye mifugo michache.
Serikali wilayani Mbarali inaendesha kampeni kabambe kuhakikisha wafugaji wanaondolewa wilayani humo na wanaokamatwa na mifugo yao wakiwa wameificha, wamekuwa wakitozwa faini.