WANAFUNZI wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto wamehoji kwa nini mahakimu wa mahakama za juu na majaji hawakamatwi kwa rushwa na badala yake wanaokamatwa ni mahakimu wa mahakama za mwanzo.
Hoja hiyo ilitolewa na wanafunzi hao wa IJA ambao wameomba Serikali kufanya utafiti ili kujua kwanini wanaokamatwa na rushwa katika ngazi za mahakama ni mahakimu wa mahakama za mwanzo tu na siyo Mahakimu wa Mahakama ngazi za juu na Majaji.
Walitoa hoja hiyo juzi wakati wa mkutano baina ya wanajumuiya ya Chuo hicho na Waziri wa Sheria na Mambo ya Katiba Dk. Mary Nagu uliofanyika ukumbi wa chuo hicho mjini hapa.
Wanafunzi hao ambao walipewa fursa ya kumuuliza maswali Waziri huyo walidai hawaoni uhalali wa kuzidi kusakamwa kwa mahakimu wa mahakama za mwanzo pekee, wakati kuna ushahidi wa mazingira kuwa wapo wakubwa wakiwamo majaji wanaojihusisha na rushwa kubwa zenye kuathiri uchumi wa nchi.
“Serikali imefanya utafiti kujua kwa nini wanaokamatwa na fedha ndogo za rushwa ni mahakimu wa mahakama za mwanzo pekee na siyo majaji,” alihoji Balisile Mwakejila mwanafunzi wa mwaka wa pili ngazi ya Stashahada na kutaka mazingira ya ufanyaji kazi ya mahakimu wa Mahakama za mwanzo yaboreshewe mafao yao.
Tumaini Mwankenja anayechukua Stashahada akiwa mwaka wa kwanza alisema watumishi wa mahakama za mwanzo wanaishi katika mazingira duni.
“Unakuta hakimu amepangiwa kazi katika eneo na hajapewa nyumba analazimika kupanga uswahilini… sasa nahoji ukiletewa kesi ya mtoto wa mwenye nyumba uliyopanga ukimfunga utaishi vipi katika nyumba hiyo?” aliuliza Mwankenja na kulalamika kuwa hapo ni lazima mazingira ya rushwa yatajitokeza.
Akijibu maswali hayo, Waziri alisema amefurahi kusikia kero za wanafunzi wa chuo hicho na kuahidi kuboresha mazingira kuanzia chuoni hadi kwenye Mahakama kwa kuwa Serikali inatambua umuhimu wao katika kuimarisha amani miongoni mwa wananchi.
Hata hivyo, alisema kuwa dawa ya kutochukua rushwa siyo kuongezewa maslahi, bali kinachotakiwa ni wao kujiengea mazoea ya kuchukia hongo kwa kuwa kufanya hivyo ni kunyang’anya haki za wanyonge.
Alisema kuwa nchi inatakiwa iendeshwe kwa misingi ya haki na sheria na siyo fedha.
Akitoa maelezo, Mkuu wa Chuo hicho Emilian Mushi alisema kina jumla ya wanafunzi 258 ambapo wanaochukua kozi ya Cheti cha Sheria wapo 53, Stashahada ya Sheria mwaka wa pili 85 na Stashahada mwaka wa kwanza 120 wakati wahadhiri waliopo ni 24.