Na Mashana Chumira, RCJ
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) Profesa Mark Mwandosya, amesema maadhimisho ya mwaka huu ya siku ya Mazingira duniani, nchini yatahusika na shughuli zinazolenga kuhifadhi misitu na vyanzo vya maji.
Profesa Mwandosya alitoa kauli hiyo jana katika mkutano na waandishi wa habari kwenye ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) kufafanua mambo kuhusu maadhimisho ya mwaka huu yanayofanyika kitaifa mkoani Singida.
Alisema lengo la kuwa na maadhimisho yenye shughuli za namna hiyo ni katika kukabiliana na vitendo vya ukataji miti ovyo usio endelevu.
Kilele cha maadhimisho hayo yaliyoanza Mei 29, itakuwa Juni 5 mwaka na mgeni rasmi atakuwa Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohammed Sheni.
"Ingawa changamoto zinazohusu mazingira ni nyingi, moja kubwa ni uharibifu wa mazingira unaotokana na ukataji miti ovyo na usio endelevu, unaotishia nchi yetu kugeuka jangwa," alisema Profesa Mwandosya.
Alitaja kauli mbiu ya mwaka huu kuwa ni "Majangwa na Kuenea kwa hali ya Jangwa" na inalenga katika kupambana na kuenea kwa hali ya jangwa nchini.
Mwanadosya alisema imeamuliwa maadhimisho hayo kitaifa kufanyika mkoani Singida kutokana na kuwa moja ya sehemu zinazotishiwa na hali ya kuenea jangwa nchini.
Siku ya mazingira duniani huadhimishwa kila mwaka kwa ujumbe maalum unaotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshugulikia Mazingira (UNEP) na unaenda na ujumbe maalum.
"Tusisababishe maeneo kame kuwa jangwa. Maudhui haya yanashabiliana na ya serikali katika kuanzisha na kutekeleza mkakati wa kitaifa wa kuhifadhi mazingira ya ardhi na vyanzo vya maji," alisema Waziri huyo.
Alisema, maadhimisho ya kitaifa husaidia katika kumhusisha kila mwananchi awe wakala mzuri wa hifadhi ya mazingira kitaifa, hasa pale alipo.
Juni 5 mwaka huu, iliamuliwa kuwa ya Mazingira Duniani kutokana na Azimio la Umoja wa Mataifa mwaka 1972, katika kikao kilichofanyika huko Stockholm, Sweden.
Uamuzi huo uliambatana na kuundwa kwa UNEP, kama chombo pekee cha Umoja wa Mataifa chenye makao makuu yake mjini Nairobi, Kenya