Na Midraji Ibrahim, Dodoma
WANAFUNZI wa Chuo Mipango na Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), wanawasiwasi kama maoni yanayokusanywa na Kamati Mchakato wa Kuelekea Shirikisho la Afrika Mashariki yatafanyiwa kazi.
Maoni hayo waliyatoa juzi kwa nyakati tofauti kwa Naibu Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Diodorus Kamala, alipokwenda kuitambulisha wizara yake kwenye vyuo hivyo.
Akichangia maoni yake, Chacha John alionyesha wasiwasi wake kuwa huenda mawazo ya wananchi ambayo watatoa hayatafanyiwa kazi na kutaka, elimu itolewe kwanza kabla ya kuanza kazi hiyo.
Wasiwasi huo, pia ulionyeshwa na wanafunzi wa Chuo cha Mipango na kueleza kuwa hali ya uelewa kwa wananchi wa vijijini ni mdogo kuhusu Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Hata hivyo, Dk Kamala aliwatoa wasiwasi huo kwamba kukusanywa kwa maoni hayo, ni hatua ya kuwashirikisha na Rais Jakaya Kikwete licha ya kukasimiwa masuala ya kusimamia haki ya Watanzania, aliona sio busara kuamua mwenye bila kushirikisha wananchi.
"Ilikuwa rahisi kujifungia vyumbani pale Arusha na kuamua kuwa sasa tunaingia kwenye Shirikisho. Lakini aliona sio busara, ndio maana tukaunda kamati ya kukusanya maoni ambayo ndio yatakuwa uamuzi wa Tanzania ingieje kwenye Shirikisho hilo,"alisema.
Dk Kamala, aliwataka wasomi hao kuacha tabia ya kubeza wananchi wa vijijini kuwa wana uelewa mdogo juu ya Afrika Mashariki na kwamba, ziara ambazo amefanya zimeonyesha kuna watu wenye hoja kuliko hata wanaojiona kuwa ni wasomi.
Baadhi ya wanafunzi pia walionyesha wasiwasi wa Watanzania kumezwa na Wakenya na Uganda, hatua ambayo inaweza kusababisha jumuiya hiyo kuvunjika tena kama ile ya awali.
Naibu Waziri huyo ambaye aliandamana na Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina, alisema suala la kuvunjika linawezekana kwa uwezo wa Mungu, lakini jumuiya mpya imejengwa kwa misingi tofauti na ile iliyovunjika na kwamba sera kuu ambayo ni muhimili hivi sasa, ni uchumi wa soko.
"Msije mkatarajia kusikia Mamlaka ya Mapato ya EAC, Shirika la Ndege la Afrika Mashariki au Shirika la Reli kama ilivyokuwa awali. Mashirika yatajengwa lakini chini ya usimamizi wa nchi husika, ikikopa ikashindwa kulipa juu yake, sio tuadhibiwe wanachama wote," alisema Dk Kamala.
Mihadhara hiyo ilihudhuriwa na Mkuu wa CBE, Severinus Hyera, Mkuu wa Chuo cha Mipango, Constantine Lufulilo na wafanyakazi wa vyuo hivyo.