Claud Gwandu na Mussa Juma, Arusha
DEREVA wengi wa daladala zinazofanya safari zake mjini Arusha wanatembea na silaha hali ambayo imesababisha askari polisi wa kikosi cha usalama barabarani kushambuliwa kwa sime na dereva wa daladala inayofanya safari zake kati ya Arusha na Kikatiti jana.
Habari zilizopatikana na kuthibitishwa na Kamanda wa polisi wa mkoa wa Arusha, Matei Basilio zinaeleza kuwa dereva na utingo walimshambulia askari saa 3.00 asubuhi jana katika barabara ya Chagga, eneo la Chini ya Mti mjini hapa baada ya askari wa usalama barabarani PC Hamad kujaribu kulikamata gari hilo.
Tukio hilo linafanyika siku chache baada ya lile la jijini Dar es Salaam ambapo dereva wa basi maarufu kama 'daladala' anadaiwa kuuawa kwa kupingwa risasi baada ya kutokea mzozo wa barabaran kati yake na aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Tabora, Ukiwaona Mzuzuri Ditopile, ambaye sasa anashikiliwa na polisi.
Watu walioshuhudia tukio la mjini Arusha walisema kuwa askari huyo alikuwa akijaribu kulikamata gari hilo kwa kosa la uendeshaji vibaya wa gari barabarani na ndipo alipokatwa mapanga begani na kifuani na kisha dereva na utingo wake wakatoroka.
Kamanda Basilio alisema kuwa msako mkali wa kuwakamata dereva na utingo wake umeanza na kuwaomba wananchi kusaidia kutoa taarifa za walipokimbilia ili wakumbane na mkono wa sheria.
“Ni kweli askari wetu,PC Hamad alikatwa mapanga na derava huyo pengine akisaidiana na utingo wake lakini tunashukuru mungu hajaumia sana na amepatiwa matibabu na kuruhusiwa kupumzika nyumbani.”
“Ni tukio la kusikitisha mno kwani askari alikuwa akijaribu kuhakikisha sheria za barabarani zinafuatwa ili kuepusha ajali zinazosababishwa na uzembe wa madereva lakini badala yake wakamkata mapanga. Tutawatafuta popote walipo ili wafikishwe mahakamani na tunaomba sana ushirikiano wa wananchi,”alisema kamanda Basilio, kwa njia ya simu jana.
Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo ambaye hakutaka jina lake litatajwe gazetini alisema kuwa alishuhudia dereva huyo akibishana na askari huyo wa usalama barabarani aliposimamishwa na ghafla akavuta sime aliyokuwa nayo na akaanza kumkata askari huyo na akakimbia.
Baada ya askari huyo kujeruhiwa huku dereva na utingo wake wakikimbia aliomba msaada kwa wenzake kwa kutumia redio ya polisi na ndipo askari hao wa usalama barabarani wakafurika katika eneo hilo na kisha kumkimbiza wenzao hospitalini.
Shuhuda alisema watu walianza kufurika katika eneo la tukio kuona nini kinaendelea lakini askari wa usalama barabarani waliendelea kuwasiliana na wakubwa wao na baada ya muda gari la askari wa kutuliza ghasia(FFU) lilifika katika eneo hilo na kuanza kuwatawanya watu.
Daladala hiyo inashikiliwa katika kituo kikuu cha polisi mjini hapa huku jitihada za kuwakamata watuhumiwa hao zikiendelea.
Katika siku za karibuni Jeshi la Polisi mkoani hapa limekuwa likichukua hatua mbalimbali za kuimarisha usafiri wa daladala ikiwa ni pamoja na kubadilisha vituo ili kupunguza msongamano mkubwa unaosababishwa na madereva wa magari hayo kuendesha ovyo wakiwa barabarani.
Uchunguzi wa Mwananchi umeonyesha kuwa madereva wengi wa magari yakiwamo daladala katika mji wa Arusha wanatembea na silaha ikiwamo sime kwa hofu ya kuvamiwa na majambazi.