Na Theonestina Juma, Bukoba
WANAFUNZI 132 wa shule ya msingi Ibosa kata ya Nyakato wilaya ya Bukoba Vijijini na Mwalimu wao mmoja wamejeruhiwa na radi shuleni baada ya mvua kubwa iliyonyesha wilayani humo.
Radi hiyo inayodaiwa kupiga kama bomu, ilisababisha hasara kubwa shuleni hapo huku ikiwa imebomoa ofisi ya Mkuu wa shule, matanki mawili ya maji pamoja na kuezua paa za madarasa ya shule hiyo.
Mwandishi wa habari hizi alishuhudia wanafunzi hao wakipakiwa kwenye magari kupelekwa hospitali ya mkoa wa Kagera mjini
hapa ambapo wazazi wao walifurika hospitalini hapo kuwajulia
hali huku wakiwa wametaharuki kuhusu usalama wa watoto wao.
Hospitalini mwandishi alikuta wauguzi na madaktari wakiwapatia huduma ya kwanza watoto waliojeruhiwa vibaya katika tukio hilo.
Kaimu Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Bi. Domina Katunzi alisema watoto wengi walijeruhiwa kutokana na radi kupasua vioo vya madirisha ya shule, matofali kuwaangukia kutokana na majengo ya shule hiyo kubomolewa kupita kiasi kufuatia mtikisiko uliotokea.
Watoto waliojeruwahi zaidi ni Gerad Daniel (17) wa darasa la sita, aliyejeruhiwa mguu na mkono, Analsius Medai (13) wa darasa la sita, Edward Leonard (12), Dominick Ludovick (16) wa darasa la nne na Julian Kabendera (16) wa darasa la sita wanaolalamika kwamaumivu ya kichwa, mkono, mguu na walilazwa wodi namba nne.
Winfrida Gervas (16) wa darasa la nne na Priska Rumalila (11) walilazwa kutokana na kuumia kichwa na mdomo wakati Mwalimu Bw. Alponce Balilemwa (54) alijeruhiwa pia katika tukio hilo.
Akizungumza na gazeti hili nje ya wodi namba 4 walikolazwa
kwa muda pamoja na wanafunzi wake, Mwalimu huyo alisema wakati radi ikipiga ilimkuta Ofisini kwa Mwalimu Mkuu akiwa na mwanafunzi mmoja ambapo jengo hilo liliharibiwa vibaya na radi hiyo kwa kung'oa mlango na kuezua paa la Ofisi ya Mwalimu Mkuu.
Hadi jana jioni, watoto hao walikuwa hawajaruhusiwa kutoka hospitalini hapo na Daktari, Bi. Katunzi alisema wanaendelea kuwapokea watoto waliojeruhiwa na haijajulikani ni wangapi ambao watalazwa kutokana na wengi wao kupata majeraha madogo kutokana na kupigwa na matofali yaliyobomolewa na radi hiyo.