Na Mwandishi Wetu
UWANJA wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, umeimarisha mfumo wake wa kupambana na majanga ili kukabiliana na matukio ya hatari yakiwamo ya ugaidi.
Katika kujiimarisha mfumo huo, mamlaka hiyo imekuwa ikifanya mazoezi ya uokoaji ya mara kwa mara kwa ajili ya kufanyia majaribio mfumo wake wa dharura.
Mazoezi hayo yanahusu pia vifaa vya ukoaji kama magari ya zima moto na yanahusisha mawasiliano ya kisasa ambayo huunganisha maeneo muhimu na vyombo vingine vya dola.
Vyombo hivyo vya dola ni pamoja na Idara ya Usalama wa Taifa uwanjani hapo, kikosi cha Jeshi na maeneo muhimu nje ya hapo kama hospitali kubwa kama Muhimbili.
Chini ya mfumo huo na mazoezi yake, mamlaka hiyo inaangalia mwitikio wa vyombo vingine vinavyopata taarifa za kutokea dharura uwanjani hapo kuona kama uko sahihi.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu ambaye pia Meneja wa Usalama Uwanja huo, Msangi Salim, alifafanua jijini Dar es Salaam jana kwamba, ingawa Tanzania haijakumbwa na majanga makubwa, lakini bado inapaswa kujijengea mfumo imara wa kukabiliana na majanga ya dharura.
"Tumejipanga kukabiliana na majanga kwa kushirikiana na wenzetu, tumekuwa tukifanya mazoezi ya mara kwa mara, tunataka kuona mwitikio wa vyombo vingine wakati wa dharura ukoje," alisema.