Na Mwandishi Wetu
MAWAKILI wanaomtetea aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Kapteni Ukiwaona Ramadhan Mwinshehe Ditopile Mzuzuri dhidi ya tuhuma za mauaji, wamekuja juu na kuwataka wananchi na taasisi mbalimbali kuacha kumhukumu mteja wao nje ya mahakama, ili kupisha vyombo husika vifanye kazi zake bila kuingiliwa.
Kapteni Ditopile anakabiliwa na tuhuma za mauaji ya dereva wa daladala, Hassan Mbonde, ambaye alipigwa risasi na kufariki dunia eneo la njia panda ya Kawe jijini Dar es Salaam.
Tukio hilo lilitokea Novemba 4, mwaka huu na tayari mtuhumiwa alishafikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam. Hata hivyo hakutakiwa kujibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusilikiza kesi za mauaji hadi atapofikishwa mahakama kuu. Imepangwa kutajwa tena katika Mahakama ya Kisutu Novemba 20, mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, mmoja wa mawakili hao, Sam Mapande, alisema tangu kutokea kwa tukio hilo, kumekuwa na maneno mengi ya uvumi kutoka kwenye taasisi mbalimbali na watu binafsi, zenye kutaka kushawishi umma uone kwamba mteja wao ametenda kosa la mauaji kama anavyotuhumiwa.
Pamoja na Mapande, mawakili wengine wa kampuni hiyo wanaomtetea Ditopile ni Dk Ringo Tenga, Cuthbert Tenga na Losan Mbwambo.
Mapande aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa matamshi, taarifa na maneno ya yanayoelekea kuishawishi jamii kuwa mtuhumiwa anayo au hana hatia, kabla hata mahakama haijasikiliza shauri hilo na kutoa uamuzi, zinamnyima mtumhumiwa haki ya kupata fursa ya kujitetea.
Alisema jambo la kushangaza ni kwamba baadhi ya taasisi zinazotoa matamshi ya aina hiyo zinaongozwa na wanasheria ambao wanajua kuwa ushahidi halali wa kile kilichotokea, unatolewa mahakamani peke yake.
Alieleza kushangazwa kwake na taasisi zinazotoa kauli zinazomhukumu mteja wake tena mbele ya vyombo vya habari wakati zikijua wazi kuwa mtuhumiwa amefikia uamuzi wa kujizulu nafasi yake ili kutoa nafasi kwa mahakama kufanya kazi yake bila kishawishi chochote.
Alisisitiza kuwa ni mahakama peke yake ndio yenye uwezo wa kusema kuwa mteja wao (Ditopile) ana hatia au hana na sio mtu au taasisi yoyote ile nje ya utaratibu wa mahakama.
Mapande alikariri kauli kadhaa za busara za watu wa zamani zinazoonyesha kuwa mahakama pekee ndiyo inayotakiwa kutoa haki katika shauri lolote na kwamba inapoingiliwa na taasisi nyingine zilizo nje ya utaratibu wake kiutendaji, uhuru wa maamuzi yake unakuwa shakani.
"Tukumbuke kwamba, Ditopile Mzuzuri si malaika ni binadamu kama mimi na wewe na sheria hakutungiwa yeye bali sisi sote. Hivyo basi mimi na wewe inawazekana kabisa ni watuhumiwa watarajiwa. Hivyo tuenende kama sheria inavyotutaka na tuviachie vyombo husika kufanya kazi zake bila kuviingiliwa," alisema Mapande
Mapande alisisitiza kuwa wataendelea kumtetea mteja wao kwa mujibu wa sheria za nchi kwa kuwa kuna kifungu cha sheria kinachomlinda kwamba mtuhumiwa hana makosa hadi pale mahakama itakapothibitisha tuhuma dhidi yake.