Na Mwandishi Wetu, Dodoma
WATU walionunua nyumba za serikali kinyemela, sasa wanakabiliwa na hatari ya kunyang'anywa kutokana na tathmini inayofanywa kuhusiana na uuzaji wa nyumba hizo.
Kumekuwapo na madai katika vyombo vya habari nchini kuwa baadhi ya watu wasiostahili, waliuziwa nyumba za serikali katika zoezi lililoendeshwa chini ya Wakala wa Nyumba za Serikali.
Tayari Wizara ya Miundombinu, ambayo ndiyo msimamizi mkuu wa nyumba za serikali, inaendesha tathmini ya uuzaji wa nyumba hizo, ikiangalia kama kuna taratibu zilizokiukwa wakati wa uuzaji wake.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari hivi karibuni, Rais Jakaya Kikwete pia alizungumzia matatizo yaliyojitokeza baada ya kuuzwa kwa nyumba hizo na kuahidi kuwa serikali ilikuwa inaangalia namna ya kuzirejesha baadhi yake.
Rais Kikwete alitoa mfano wa nyumba za wakuu wa polisi wa wilaya ambazo zimejengwa kwenye maeneo ya polisi ambazo ziliuzwa kwa watu, akisema inakuwa vigumu kwa raia wa kawaida kuishi ndani ya eneo la polisi.
Naibu Waziri wa Miundombinu, Dk Makongoro Mahanga, aliliambia Bunge jana mjini hapa kuwa watu waliopata nyumba hizo kwa mlango wa nyuma, wataumbuka baada ya tathmini ya zoezi hilo kukamilika.
Dk Makongoro Mahanga, alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Kalenga (CCM), Stephen Galinoma, aliyetaka kujua msimamo wa serikali kuhusiana na uuzaji wa nyumba hizo na kama zoezi hilo litaendelea miaka ijayo.
Mbunge huyo alisema mchakato mzima wa uuzaji wa nyumba hizo umejaa utata na pia kumekuwapo na baadhi ya kauli za viongozi wa serikali zinazopingana, hivyo, akaishauri serikali iunde tume kuchunguza kasoro zilizojitokeza wakati wa uuzaji nyumba hizo ili ziweze kurekebishwa.
Dk Mahanga alisema kuwa matokeo ya tathmini hiyo, yataisaidia serikali kuboresha udhaifu uliojitokeza wakati wa utekelezaji wa zoezi hilo.
Alisema pale ambapo utaratibu haukufuatwa wakati wa utekelezaji wake, hatua zitachukuliwa kurekebisha hali hiyo, ikiwamo kuzirudisha serikalini nyumba kama hizo.
Hata hivyo, Mahanga ambaye pia ni Mbunge wa Ukonga (CCM), alisisitiza kuwa, serikali ya awamu ya nne haipingani na maamuzi ya awali ya kuuza nyumba hizo, bali itahakikisha kuwa nyingine zitakazojengwa au kutengwa kwa ajili ya viongozi na watumishi wengine wenye stahili, haziuzwi tena.
“Kubwa katika maamuzi ya serikali ya awamu ya nne ni kusisitiza maamuzi ya awali kwamba baada ya nyumba zilizoamuliwa kuuzwa, nyumba zingine zitakazojengwa rasmi au kutengwa kwa ajili ya viongozi na watumishi wengine wenye stahili hazitauzwa, ” alisisitiza Dk Makongoro.
Alisema kuanzia mwaka 2001, serikali iliamua kuuza baadhi ya nyumba zake kwa watumishi wa umma kwa lengo la kuwaezesha kupata makazi bora wakati wakiwa kazini na baada ya kustaafu.
Dk Mahanga alisema uamuzi wa kuuza nyumba hizo, ulifikiwa ili kuondokana na gharama kubwa ya kuzifanyia matengenezo na fedha ambazo zitapatika kutokana na uuzaji huo ziweze kutumika kujenga nyumba nyingine ili kupunguza tatizo la makazi kwa watumishi wa umma.