Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
KAMISHNA wa Polisi Zanzibar, Khalid Idd Nuizani amemtunukia cheo Koplo Hafidh Ali Mgeni wa Kituo cha Polisi Ng’ambona kuwa Sajini kwa kuzuia bendera ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kuanguka mbele ya Rais Aman Abeid Karume.
Askari huyo aliizua bendera hiyo kuanguka kwa kudaka mlingoti uliokuwa unaanguka baada ya kuelemewa na upepo.
Tukio hilo lilitokea hivi karibuni wakati Karume akihutubia mkutano wa hadhara katika uwanja wa Aman, kuadhimisha sherehe za 'elimu bila malipo'.
Kamishna Khalid alimzawadia cheo hicho kwa niaba ya Inspekta Jeneral wa Polisi ( IGP), Said Mwema, mbele ya makamanda na askari wa vyeo mbalimbali wa mikoa mitatu ya Unguja katika ukumbi wa Ziwani.
Vile vile ilielezwa kuwa Sajini Meja Rashid Zam na Koplo Ramadhan watapewa kipaumbele kwa mapendekezo ya kujiunga na kozi zijazo.
Akizungumzia ajali za barabarani, Kamishna Khalid alisema tatizo hilo limezidi kuongezeka hivyo polisi wanapaswa kuongeza nguvu ya kudhibiti na kuchukua hatua za kisheria dhidi ya wanaosababisha ajali hizo.
Kuhusu ujambazi ulioibuka kwa kasi kuanzia Julai mwaka huu, aliomba ushirikiano wa raia ili kuwezesha mapambano dhidi yake kufanikiwa kwa kuwa jeshi hilo linawajibika kuhakikisha usalama wa watalii wanapotembelea nchini kwani ni kati ya sekta zinazotegemewa na serikali kwa asilimia 20 ya mapato ya taifa.