Na Mwandishi Wetu
MIEZI miwili baada ya kuripotiwa kuwapo kwa ufisadi katika Uwanja wa Ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, askari polisi 16 na afisa mmoja kutoka uwanja huo wamehamishwa vituo vya kazi. Uchunguzi umeonyesha kuwa askari hao wamehamishwa ikiwa ni moja ya jitihada za Idara ya Polisi kujaribu kusafisha uozo uliodaiwa kufanyika uwanjani hapo. Baadhi ya askari waliohamishwa (majina tunayo), walikuwa wakikabiliwa na kesi za utovu wa nidhamu ambazo zimefunguliwa katika mahakama ya kijeshi iliyokuwa ikiendesha shughuli zake katika uwanja wa ndege wa zamani (Terminal one).
Askari hao walikuwa wamefunguliwa kesi za kujihusisha na vitendo vya ukiukaji wa maadili ya kazi zao, ikiwa ni pamoja na kusaidia kupitisha abiria wanaoingia na mali za magendo na dawa za kulevya. Vile vile, walikuwa wakituhumiwa kupora abiria mizigo na stakabadhi zao zinazoonyesha kwamba wamelipa ushuru wa mizigo yao, ikiwa ni njia ya kuwalazimisha watoe rushwa. Kamanda wa Polisi, Kikosi cha Viwanja vya Ndege nchini, Halima Kiponza, alithibitisha kuhamishwa kwa askari hao na kueleza kuwa ni uhamisho kutoka makao makuu ya jeshi hilo. Alipoulizwa ikiwa kuna uhusiano kati ya uhamisho huo na tuhuma zilizokuwa zikiwakabili baadhi ya askari hao, Kamanda Kiponza alisema,"Siwezi kuthibitisha, lakini nadhani ni uhamisho wa kawaida tu." Kiponza alisema mahakama ya kijeshi iliyokuwa ikisikiliza kesi dhidi ya askari wanaotuhumiwa kujihusisha na vitendo visivyoendana na maadili ya jeshi hilo imekamilisha kazi yake. Hata hivyo, alisema uhamisho wa askari hao ambao wengi wao walikuwa ni watuhumiwa, hauna uhusiano na umauzi wa mahakama hiyo. Kuhamishwa kwa kundi hilo la askari kumefanyika miezi michache tangu gazeti la Mwananchi lifichue vitendo vya ufisadi vilivyokuwa vikifanyika uwanjani hapo kwa muda mrefu.
Hata hivyo, uhamisho wa askari hao umebezwa na baadhi ya polisi wema na maafisa usalama katika uwanja huo, kwa maelezo kwamba kuwahamishia vituo vingine ni uamuzi wa kisiasa. Kwa mujibu wa uchunguzi wa Mwananchi, askari wengi waliohamishwa majina yao yamo kwenye taarifa iliyowasilishwa kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Saidi Mwema, iliyokuwa ikituhumu utendaji kazi wao. Taarifa hiyo ya siri ambayo gazeti hili lilipata nakala yake, ilipendekeza kuhamishwa kwa baadhi ya askari katika kile kilichoelezwa kwamba ni kuimarisha usalama katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere. Miezi miwili iliyopita, gazeti la Mwananchi liliripoti kuwa baadhi ya askari polisi katika uwanja huo, mbali ya kusaidia kupitisha abiria wanaoingia na mali za magendo, pia wanafanya kazi hiyo kwa baraka kutoka baadhi ya wakubwa wa kikosi cha Jeshi la Polisi Viwanja vya Ndege.
Vigogo hao wa polisi walikuwa wanawafumbia macho vijana wakiendesha ufisadi wa kutisha uwanjani hapo bila kuwachukulia hatua zozote za kinidhamu. Mathalani, mpema mwaka huu, katika tukio moja, askari mpelelezi (jina tunalo) alimnyang'anya abiria stakabadhi za mizigo yake alizopewa baada ya kulipia ushuru wa forodha uwanjani hapo akitaka apatiwe 'chochote.' Pamoja na abiria huyo kumweleza askari huyo kuwa asingeweza kumpatia fedha kwa sababu hakuona sababu ya kufanya hivyo, askari huyo aliamua kumyanyang'anya stakabadhi za mizigo yote pamoja na tukio hilo kuripotiwa katika Kituo cha Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, hakuna hatua zilizochukuliwa dhidi ya askari huyo.
Mei 5, mwaka huu, abiria mwingine (jina tunalo) aliyekuwa ameingia nchini kutoka nje ya nchi, alilazimika kutoa rushwa ya Sh20,000 ili aachiwe baada ya kukamatwa na askari polisi (jina linahifadhiwa ) bila ya sababu zozote. Baada ya askari huyo kuhojiwa alidai kwamba suala hilo lilikuwa likijulikana na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI). Ushahidi mwingine unaonyesha kuwa Aprili 23, mwaka huu, mkazi wa Ukonga jijini Dar es Salaam (jina tunalo) ambaye alikuwa akitokea Dubai, alinyang'anywa dola za Marekani 1,000 na askari wawili (majina tunayo) na suala hilo lilijadiliwa katika kikao cha kamati ya usalama uwanjani hapo cha Mei 2, mwaka huu.