ANANCHI wa kijiji cha Isaba kata ya Kirando wilayani Nkasi mkoani Rukwa wameilalamikia Idara ya Elimu kwa kushindwa kuwapelekea walimu katika shule ya msingi Isaba yenye walimu wawili.
Malalamiko hayo waliyatoa juzi katika mkutano wa hadhara ulioitishwa na mbunge wa jimbo la Nkasi, Ponsian Nyami alipokwenda kuwashukuru kwa kumchagua katika uchaguzi mkuu uliopita.
Walidai kuwa shule hiyo ambayo ina zaidi ya miaka 24 tangu ianzishwe ina jumla ya walimu wawili ambapo mmoja kati yao alishutumiwa kwa kutowafundisha wanafunzi ipasavyo kutokana na kusafiri mara kwa mara.
Walisema shule hiyo ambayo ilianzishwa mwanzoni mwa miaka ya 1982 ikiwa na walimu watano, lakini kadri siku zilivyozidi kwenda walimu hao wamekuwa wakipungua kwa kuomba uhamisho na kuhama katika kijiji hicho, hali iliyosababisha shule hiyo kubakiwa na walimu wawili tu.
Walisema kila wakitoa malalamiko yao katika Idara hiyo wilayani, hakuna jambo lolote linalotekelezwa zaidi ya kuambiwa kuwa wilaya ya Nkasi ina upungufu mkubwa wa walimu na kwamba hawajui lini tatizo hilo litapungua au kuisha kabisa.
Kwa upande wa mwalimu mkuu wa shule hiyo, Godfrey Sumba alikiri kuwapo kwa upungufu wa walimu na kuongeza walimu hao waliopo hulazimika kuwafundisha wanafunzi 256 wa darasa la kwanza hadi la saba.
Naye Mratibu wa Elimu Kata ya Kirando A. Albart Madeni alisema kuwa kata hiyo inahitaji walimu 94 na waliopo ni walimu 39 na kwamba ina upungufun wa walimu 55 na hiyo ni kutokana na wilaya kupewa mgao mdogo wa walimu, na mwaka huu wilaya ilipewa walimu 14 na kuwafukuza kazi walimu 14 kutokana na utovu wa nidhamu
Alisema kata hiyo ya Kirando A ina jumla ya shule za msingi sita na kuzitaja shule hizo kuwa ni Kirando, Itete, Chongo Katete, Isaba, Mpata pamoja na Mtakuja.
Kutoka gazeti la Uhuru
ISSN 0876-3896 NA.19322
Na Elizabeth Maoni, Sumbawanga