Na Mwandishi Wetu KITUO Cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kinatarajia kufungua kesi ya kikatiba kutaka kumwondolea mamlaka Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) ya kufuta kesi bila sababu za msingi.
Tayari maandalizi ya ufunguaji kesi hiyo yamekwisha kufanyika na kwamba sasa yako katika hatua za mwisho.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Hellen Kijo-Bisimba, alisema lengo la kufungua kesi hiyo ni kujaribu kuziba mianya ya DPP kutumia madaraka yake vibaya kwa kufuta kesi za vigogo au watoto wao.
Mkurugenzi huyo wa LHRC, ambaye kituo chake kilishiriki kikamilifu katika kuhakikisha sheria ya takrima katika uchaguzi inafutwa, alisema kituo hicho kwa kushirikiana na wanaharakati wengine ambao hakupenda kuwataja, wanajipanga ili kuhakikisha kesi hiyo haipingwi kabla ya kufikishwa mahakamani.
Mkurugenzi huyo alisema lengo ni kuhakikisha kuwa kama DDP anafuta kesi, basi kunakuwa na sababu za msingi ambazo zinatolewa kwamba kwa nini alifuta kesi sio kufuta bila kutoa sababu.
Aliongeza kwamba DPP akifuta kesi, kisha akatoa sababu za msingi, itakuwa ni vema zaidi kwani itaondoa maswali kwa wananchi kwamba kesi fulani imefutwa kwa sababu zipi.