Na Daniel Mjema, Moshi
IDARA ya Uhamiaji mkoani Kilimanjaro, imesema raia watano wa kigeni wanaofanya kazi katika kampuni ya Kilimanjaro Plantation Ltd (KPL), wana vibali halali vya kufanya kazi nchini.
Ofisa Uhamiaji wa Mkoa, Abdullah Hamisi Abdulah, alisema mwishoni mwa wiki iliyopita kuwa, raia hao wa kigeni walipewa vibali vya kuishi na kufanya kazi nchini na Ofisi ya Uhamiaji jijini Dar es Salaam.
Abdulah alikuwa akijibu madai ya baadhi ya wafanyakazi wa kitanzania katika kampuni hiyo, ambayo zamani ilijulikana kama Tchibo Estates, kuwa raia hao wa kigeni hawana vibali vya kufanya kazi nchini.
Alifafanua kuwa mmoja kati ya raia hao, Ralph Medoch ambaye ni Mkurugenzi wa Uendeshaji ana kibali daraja A kinachotolewa kwa wawekezaji na waliobaki wanavibali daraja B.
Kampuni ya KPL imewekeza mamilioni ya dola za Marekeni 5 milioni kwa ajili ya kufufua zao la kahawa katika mashamba makubwa.
Kulikuwa na madai kuwa tume iliyoundwa na Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Mohamed Babu kuchunguza malalamiko ya wafanyakazi, iligundua pia kuwa baadhi ya raia hao hawakuwa na vibali.
Akizungumza na waandishi wa habari, Meneja Mkuu wa KPL, Peter Gethi alikanusha madai hayo na kusisitiza kuwa wanatambua na kuheshimu sheria za nchi na hawawezi kufanya kosa kama hilo.
Katika hatua nyingine, Idara ya Uhamiaji mkoani hapa, katika kipindi cha kuanzia Januari mwaka huu hadi sasa imefanikiwa kunasa wahamiaji haramu 34, walioingia nchini bila kufuata sheria.
Ofisa Uhamiaji wa Mkoa alibainisha jana kuwa wahamiaji hao walitoka nchi za Kenya, Pakistani, Ethiopia na Somalia ambao alisema walirudishwa walikotoka.
Hata hivyo, alisema Idara yake inakabiliwa na uhaba wa watumishi wa kuendesha operesheni hiyo pamoja na vitendea kazi,hivyo kuifanya idara hiyo kufanya kazi katika mazingira magumu.
Alifahamisha kuwa wakati wa operesheni wanatakiwa watumishi30, lakini ofisi yake ina watumishi wanane tu ambao wanatakiwa kukagua mahoteli, nyumba za kulala wageni na vituo vya mabasi kila siku.