Na Mwandishi Wetu, Tanga
SERIKLI imewataka wakuu wa wilaya, kujiweka tayari kwa kuwa itaendesha zoezi la kutathimini wilaya na mikoa itakayomudu kutekeleza ipasavyo, malengo yake kwa kuzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2025.
Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Mizengo Pinda alidokeza hayo wakati akifungua mafunzo ya siku 12 ya wakuu wa wilaya 27 wapya, yanayoendelea katika Hoteli ya Mkonge jijini hapa.
Aliwataka viongozi hao wakae wakijua kuwa, itafanyika tathmini hiyo ambayo itakuwa ni sawa na mashindano yatakayoiwezesha wizara kuzitambua wilaya na mikoa itakayomudu kutekeleza dira hiyo na ile itakayoshindwa.
Alisema serikali ipo katika mageuzi makubwa ya sekta ya umma na utendaji wa serikali za mitaa, mageuzi ambayo yanahitaji serikali kuu na za mitaa kuwa na vigezo vya utendaji vinavyopimika kwa kila malengo inayojiwekea.
“Tusipofanya tathmini kama hiyo, hatuwezi kujua wapi tumefanikiwa, wapi kuna vikwazo vinavyotakiwa kuondolewa na wapi uongozi uwe wa wilaya au mkoa umezembea,” alionya Pinda.
Waziri Pinda alisema, wajibu na majukumu ya mkuu wa wilaya ni lazima yatekelezwe kwa kuzingatia malengo ya ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2025, kama msingi na mwongozo wa sera.
Alisema dira hii inaonyesha malengo na meneo mbalimbali ya utekelezaji na ambayo yanaunganisha jitihada mbalimbali za kupunguza umasikini, ili kuboresha maisha ya wananchi, kuendeleza utawala bora na kujenga uchumi imara na endelevu.
Mafunzo hayo elekezi ya wakuu wa wilaya wapya, yalifunguliwa kwa wakati mmoja katika vituo vya Tanga na Tabora ambako wameshiriki wakuu wa wilaya 21, lengo likiwa ni kuwapiga msasa juu ya kazi zinazowakabili katika vituo vyao vya kazi.