Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
KUNDI la watu wanane wanaosadikiwa kuwa ni majambazi juzi usiku wamewashambulia watu tisa kwa mapanga, walipokuwa wanasafiri katika mashua kutoka Zanzibar kwenda Dar es Salaam.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Bakari Khatib Shaaban, alisema jana kuwa katika tukio hilo, watu watatu walipata majeraha na kutibiwa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja na baadaye kuruhusiwa.
Majambazi hao, alisema, walifanikiwa kuiba vitu kadhaa pamoja na fedha taslim,Sh300,000.
Vitu vingine vilivyoporwa pamoja na katoni 100 za betri katuni, televisheni sita, sukari mifuko minne, katoni 20 za maziwa ya makopo na simu tano za mkononi.
Kamanda Bakari alisema tukio hilo lilitokea saa 5.00 usiku wa kuamkia jana, baada ya mashua hiyo kukaribia kisiwa cha Chumbe, kilomita chache kutoka bandari ya Zanzibar.
Alisema watu hao waliokuwa na mapanga na visu, waliwatishia abiria hao na kisha kuwapora. Mpaka sasa watu waliohusika na vitendo hivyo bado hawajakamatwa na polisi inaendelea na uchunguzi.
Aliwataja watu walioshambuliwa kuwa ni Nahodha wa chombo, Haji Ali Sheha (45), Mohamed Ali Mohamed, Hassan Waziri Moshi, Shaaban Mussa Mizenga, Stumai Nassor Mussa, Ali Yahya Jalala, Masoud Mmaka Mohamed, Omar Hamad Juma na Edward Mshimba Florence.
Kamanda Shaaban aliwaomba wananchi kutoa ushirikiano ili kufanikisha kukamatwa kwa majambazi hao na kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria.
Aliwataka watu kuchukua tahadhari wakati wanaposafiri kati ya Zanzibar na Dar es Salaam kwa usiku kwa kuhakikiha kuwa, vyombo wanavyopanda vimeandikishwa na kuruhusiwa kihalali.