MBUNGE wa Kibiti Abdul Marombwa ametoa wito kwa wananchi wa jimbo hilo kuyapa kipaumbele mazao ya korosho na ufuta ili kukuza uchumi na kupunguza umasikini.
Marombwa ametoa wito huo kwenye mikutano ya hadhara katika vijiji vya kata za Matunda, Ruaruke, Mchukuvi, Mahege na Kibiti.
Alisema, malumbano ya kisiasa kwa wakati huu yamekwisha na kilicho mbele ya wananchi kwa sasa ni kuwa na mshikamano katika kazi za kukuza uchumi na kupunguza umaskini.
Mbunge huyo alisema, maendeleo yanakwenda pale ambapo watu wake wanapenda maendeleo na kusisitiza kuwa bila kujishughulisha kamwe maendeleo hayawezi kunyesha kama mvua.
Aidha, Marombwa aliwahimiza wananchi kutilia mkazo kilimo cha korosho na kuwahakikishia wakulima upatikanaji wa pembejeo kwa wakati.
Akiwa kwenye kijiji cha Mlanzi, mbunge huyo aliwataka wananchi kutunza na kutumia vizuri vyakula wanavyovuna na waondokane na uchezaji ngoma holela.
Wanakijiji wameshasafisha eneo la ekari 22 na wameshafyatua matofali 4,000 kwa ajili ya ujenzi wa shule ya sekondari kijijini.
Kutoka gazeti la Uhuru
ISSN 0876-3896 NA.19322
Na Selemani Ndumbogani, Rufiji