Na Hussein Issa, Mtwara
UONGOZI wa Gereza la Namajani, Wilayani Masasi, Mkoa wa Mtwara umeshauriwa kuliachia eneo kubwa la ardhi wanalomiliki na kuwapa wananchi ambao watalitumia kwa kilimo.
Mbunge wa Masasi, Raynald Mrope (CCM) aliiambia Mwananchi Jumapili katika mahojiano maalum kuwa gereza hilo linamiliki eneo kubwa ambalo halitumiki na kuliacha likiwa pori huku wananchi wakihangaika kutafuta sehemu ya kulima.
“Nashangaa sana kuona Magereza wanamiliki eneo kubwa mno ambalo nina hakika halitumiki sasa kwanini wasiachie wananchi walitumie katika harakati za kujiepusha na adha hii ya njaa," alisema Mrope.
Hata hivyo, alishukuru juhudi za serikali kuingilia kati suala hili kati kwa ajili ya kuwawezesha wananchi wa Masasi kupata ardhi na kuepuka na njaa inayotokana na ukosefu wa mashamba huku kukiwa na ardhi isiyoendelezwa.
Mbunge huyo aliongeza kuwa wananchi hao hawataki kutumia eneo lote, isipokuwa sehemu kwa ajili ya kulima mazao au hata mboga mboga za muda mfupi nasio kulimiki eneo la gereza kama wanavyodai viongozi wa gereza hilo.
Aliwataka viongozi hao waachie sehemu ndogo ambayo hawaitumii kwa wananchi kuwapa nafasi ya kilimo.