Na Noor Shija, Tokyo , Japan
RAIS Jakaya Kikwete amefafanua kuwa Tanzania inahitaji wawekezaji kutoka duniani kote, lakini amesisitiza kwamba wawape kipaumbele katika ajira Watanzania wenye uwezo ambao ni wengi, badala ya kufikiria kuwapa ajira watu wanaotoka katika nchi zao.
Rais Kikwete alitoa ufafanuzi huo kufuatia taarifa iliyonukuliwa kimakosa na gazeti hili kwamba amewakataa wawekezaji kutoka India na Pakistan.
“Siyo kwamba hatuwataki wawekezaji kutoka India na Pakistan, nilichosema ni kwamba Tanzania kumejaa wawekezaji kutoka India na Pakstan, lakini bado hawatoshi. Tunahitaji wawekezaji zaidi kutoka duniani kote, lakini nasisitiza kuwa watoe kipaumbele cha ajira kwa Watanzania wenye uwezo wa kufanya kazi hizo,” alisema Rais.
“Tanzania inahitaji wawekezaji wengi kutoka Japan ili kuongeza ajira na kuwajengea uwezo Watanzania zaidi,” alisema katika ufafanuzi wa mazungumzo yake na mtaalamu wa uchumi wa Japan, Dk. Shoichi Kobayashi.Kobayashi ndiye aliyeandika mpango ‘Min Tiger 2020’ ambao unalenga kukuza pato la Mtanzania kutoka dola 375 za Marekani kwa mwaka za sasa hadi dola 1,500 kufikia mwaka 2020 na kukuza pato la taifa toka dola bilioni 10 kwa sasa hadi dola bilioni 40 mwaka 2020.
Rais Kikwete alisema Tanzania ina wawekezaji wengi kutoka bara Asia, zikiwemo India na Pakistan, “lakini tungependa na Wajapan nao waje kwa wingi ili kuweza kufikia malengo ya kuondoa umasikini”.
Rais alibainisha kuwa kuna bidhaa kutoka Japan, lakini sasa Tanzania inahitaji wawekezaji wa kuwekeza katika sekta mbalimbali, hasa viwanda, ili kutoa ujuzi na ajira nyingi kwa Watanzania kwa lengo la kuinua uchumi wa Mtanzania.
Rais Kikwete jana alimaliza kutembelea Japan na leo anakwenda China kuendelea na ziara ya kikazi ya kujitambulisha na kutafuta wawekezaji.