Na Noor Shija, Tokyo, Japan
MKE wa Rais, Mama Salma Kikwete amesisitiza kuwa mahusiano mazuri baina ya wanafunzi na walimu yanamjengea mwanafunzi msingi mzuri wa elimu.
Alisema hayo wakati akizungumza na walimu na wanafunzi mara baada ya kutembelea shule ya msingi ya Bancho, mjini Tokyo, iliyofunguliwa miaka 135 iliyopita.
Mama Salma alisema ushirikiano shuleni utawasaidia wanafunzi kushika na kuendeleza mambo mbalimbali wanayofundishwa wakiwa darasani.
“Shule ya msingi ndiyo mahali ambapo watoto wanatayarishwa kuwa viongozi wazuri wa baadaye na raia wema kwa taifa lolote, hivyo ni bora kukawa na mahusiano mazuri baina yao na waalimu,” alisema.
Wakati wa ziara hiyo, Mama Salma alitembelea darasa la sayansi ambapo alishuhudia watoto wanavyotayarishwa kuipenda elimu ya sayansi kwa kufundishwa kwa vitendo mambo yanavyoweza kubadilika kutoka uasilia wake na kuwa katika mfumo mwingine.
Alitumia wakati huo kuishukuru serikali ya Japan kwa misaada inayotoa kwa Tanzania, hasa katika sekta ya elimu, ambayo alisema hivi sasa imeboreshwa zaidi.
Shule ya msingi ya Bancho imewahi kutembelewa na Mama Maria Nyerere, mke wa Rais wa kwanza wa Tanzania, Baba wa Taifa, marehemu Mwalimu Julius Nyerere.