Na Jane Mihanji, Morogoro
MGANGA Mkuu wa mkoa wa Morogoro Dk. Meshack Massi amesema anawasiliana na Bohari Kuu ya Dawa (MSD) kuangalia uwezekano wa kuleta vifaa bora kwa ajili ya chumba cha upasuaji.
Dk. Massi aliyasema hayo baada ya kuulizwa na Uhuru ni vipi mkoa utalitatua tatizo la hali duni ya chumba cha upasuaji ambapo Naibu Waziri wa Afya Dk. Aisha Kigoda alifanya ziara katika hospitali ya mkoa na kubaini tatizo hilo.
"Unajua vifaa vingine tuliletewa ubora wake haukuwa mzuri...tunawasiliana na Bohari Kuu kuangalia uwezekano wa kuleta vifaa bora zaidi," alisema Dk. Massi.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Dk. Massi katika taarifa yake kwa Naibu Waziri wa Afya alilalamikia hali duni ya vifaa vinavyoletwa na bohari kuu au kutopatikana kabisa kwa vifaa na hata dawa.
Alitoa mfano wa hospitali ya mkoa kushindwa kufanya kazi kwa ufasaha hasa pale wanapotokea wagonjwa wa ajali kwa kukosa dawa, sindano ya Mannitol ambayo hupunguza hali ya mshtuko unaosababisha maumivu makali kwa mgonjwa.
"Dawa hii tumeiomba sana bohari kila kukicha watakujibu majibu mazuri sana. Tumeishiwa tumeiagiza Afrika Kusini,|"alisema Dk. Massi na kushauri kuwa ingekuwa vema bajeti ya dawa inayotolewa na serikali na kupelekwa moja kwa moja bohari ya dawa sasa ipelekwe katika hospitali ili waweze kununua wenyewe baadhi ya vifaa.
Dk. Massi alisema kwa kufanya hivyo huenda kukawa na ushindani kidogo na bohari ya dawa kujitahidi kupata vifaa bora zaidi.
Akizungumzia kuhusu muuguzi anayetuhumiwa kuomba hongo ya sh. 500, alisema ofisi yake imetoa maelekezo kwa uongozi wa hospitali ya mkoa ili hatua zaidi zichukuliwe.
Alisema jana katika kikao cha kawaida cha kila siku asubuhi waliwaonya watumishi na kuwataka nao pia waonyane kuacha tabia ya kuomba fedha wanapotoa huduma.
Kutoka gazeti la Uhuru