MADAKTARI wawili raia wa Tanzania wamefariki dunia katika ajali ya ndege iliyotokea Abuja nchini Nigeria Oktoba 29.
Madaktari waliofariki dunia katika ajali hiyo wametajwa kuwa ni Dk. Nakijwa Kanyika wa Hospitali ya Mkoa wa Morogoro na Dk. Moshi Ruhiso wa Hospitali ya Makandana ya Wilaya ya Rungwe, mkoani Mbeya.
Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa inaeleza kuwa, Watanzania hao waliwasili nchini Nigeria Oktoba 27 kwa shughuli za kikazi zilizokuwa zikiratibiwa na Shirika la Afya Duniani (WHO).
“Maiti za Watanzania hao zilitambuliwa na Watanzania wenzao, Dk. Esther Mwakitalu pamoja na Dk. Harriet Hamis, ambao waliongozana nao huko Nigeria. Hao walibaki Lagos kwa ajili ya kwenda jimbo jingine,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Mipango ya kuisafirisha miili ya Watanzania hao inafanywa na Ubalozi wa Tanzania nchini Nigeria kwa kushirikiana na WHO. Miili hiyo inatarajiwa kuondoka Abuja leo kuja Dar es Salaam.
“Serikali imesikitishwa na vifo hivyo na imetuma rambirambi kwa familia za marehemu, ndugu, jamaa na marafiki waliofikwa na msiba huo,” ilieleza sehemu ya taarifa.
Ndege ya abiria aina ya Boeing 737 ilianguka Oktoba 29 ikiwa ni muda mfupi baada ya kupaa kuelekea katika Jiji la laskazini la Sokoto nchini Nigeria.
Katika ajali hiyo, watu 100 walifariki ambapo watu sita wanadaiwa kunusurika na taarifa zaidi zinasema kuwa Rais wa Nigeria, Olusegun Obasanjo ameagiza kuanza kwa uchunguzi wa ajali hiyo