WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Maafa na Ukimwi), Dk. Luka Siyame, amesema serikali imeshindwa kuhamia Dodoma kutokana na kuwapo kwa upungufu katika sheria ya ujenzi wa Makao Makuu.
Alisema kutokana na hali hiyo, hivi sasa serikali inafanya jitihada za kuifanyia marekebisho sheria hiyo, ikiwa pamoja na kuboresha sheria ya uwekezaji, kuondoa kasoro kadhaa na kuipa sura mpya inayoendana na mazingira ya sasa.
Kauli hiyo ya Siyame imekuja ikiwa ni miaka takriban 40 sasa, tangu mpango wa kuhamishia makao makuu kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma ulipobuniwa na Serikali ya Awamu ya Kwanza.
Dk. Siyame aliliambia Bunge jana mjini hapa, alipokuwa akijibu swali la mbunge wa Dodoma Mjini, Ephraim Madeje (CCM), aliyetaka kujua serikali imefikia wapi kukamilisha ujenzi huo na hatimaye kuhamishia shughuli zake hapo.
Alisema utekelezwaji huo umekwama kutokana na upungufu wa sheria hiyo, vikiwamo vifungu namba 13 na 11 vilivyohusu unafuu wa asilimia 50 katika gharama za maji na umeme.
Alisema upungufu mwingine ni kwenye kifungu namba 16 cha sheria hiyo kuhusu nafuu katika biashara zilizoainishwa ambayo inatoa tafsiri zenye maana nyingi.
Kasoro nyingine ni kutokuwapo kwa kampuni tanzu za Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA), zilizolenga kupata msamaha wa kodi ya mapato na kutoa mchango mkubwa katika uendelezaji wa mji huo.
“Mamlaka hizo zimefilisiwa na serikali kutokana na sera ya serikali kujitoa katika biashara sambamba na kutokuwa na majukumu ya kampuni hizo,” alisema Waziri Siyame.
Wakati serikali ikitoa majibu hayo, taasisi kadhaa za umma zikiwamo wizara, zimeendelea kujenga majengo ya kisasa na yenye hadhi ya kuwa makao makuu ya ofisi zao jijini Dar es Salaam hali inayoonyesha kukosekana kwa dhamira ya kweli ya kupeleka makao makuu Dodoma, azma ambayo ilianzishwa miaka ya 1960 na wazo la kuundwa kwa CDA likaja mwaka 1969 na ikaanzishwa rasmi mwaka 1973.
Sambamba na hilo, taasisi za kimataifa zikiwamo balozi kama ile ya Jumuiya ya Ulaya na kabla ya hapo, ubalozi wa Marekani, zote zimeendelea kujiimarisha kimajengo na kimakazi jijini Dar es Salaam, hali inayoonyesha kwamba nazo zimekuwa hazioni jitihada za wazi za serikali kuhamia Dodoma.