Mtanzania mwenzangu,
Kwa mtazamo wa kawaida na wa kijuujuu,watanzania tunajulikana kwa kuwa wazalendo sana. Tunasemekana kuwa watu tunaoipenda nchi yetu na tunaojipenda pia. Tumejipa majina kemkem katika kujivunia utanzania wetu. Nchi yetu inajulikana miongoni mwa wengi kama “bongo” yaani akili.
Zamani zile “bongo” ilikuwa ni jiji la Dar-es-salaam tu,siku hizi bongo ni Tanzania nzima au niseme Tanganyika nzima ingawa najua kuna watu wanajidai kwamba jina Tanganyika halimo katika msamiati wao. Huko ni kujidanganya na kupotosha historia.
Kwa wengi, ingawa sera za kiuchumi za Mwalimu Nyerere zilifeli,sera za kijamii zilifanikiwa sana. Mojawapo ya mafanikio ya kijamii ni pamoja na hili la “uzalendo”.Mapenzi yasiyo kifani kwa nchi yetu,popote tulipo tunaiota Tanzania nk.
Leo nataka niangalie kidogo kama kuna ukweli wowote kwamba tunaipenda sana nchi yetu. Lakini kabla sijaenda mbele sana naomba niweke wazi kwamba mimi siamini kama tunaipenda kweli nchi yetu kama tunavyodai. Naona tunashabikia nchi yetu lakini hatuipendi nchi yetu.
Kwani nchi ni nini basi? Nchi ni mbuga za wanyama? Nchi ni maeneo ya kijografia aliyotuwekea mkoloni? Nchi ni mashamba yasiyozalisha? Tafsiri ya nchi inaweza kuwa ngumu sana, kila mtu anaweza akawa na tafsiri yake na kila mmoja akawa sawa.Kwangu mimi nchi ni yote hayo hapo juu na mengineyo pamoja na watu wake. Sipati picha na “nchi” bila watu.
Nchi yetu ipo ilipo kwa sababu ya ukosefu wa “uzalendo”.Tofauti na madai ya wengi wetu,mapenzi (uzalendo) kwa nchi yetu ni kama hakuna. Kama unaipenda nchi yako,utaiibia? Kama unaipenda nchi yako utakula rushwa? Kama unaipenda nchi yako hutoonyesha wazi bali mpaka utolewe kashfa ndio uzinduke? Kama unaipenda nchi yako utakwepa kodi? Kama unaipenda nchi yako utakuwa mzembe kazini? Kama unaipenda nchi yako utaloga wenzako?
Kama unaipenda nchi yako utaacha kuichagulia viongozi bora na sio kwa kusubiri upewe rushwa? Kama unaipenda nchi yako utaikana? Kama unaipenda nchi yako utaachia wageni waje na kuchuma uchumi wote wa nchi ilhali wewe umekaa tu kibarazani?
Kama unaipenda nchi yako utakuwa huijui hata historia yake achilia mbali jiografia yake? Kama unaipenda nchi yako utajifanya huijui hata lugha rasmi ya nchi yako ili mradi uonekane bora miongoni wa kundi fulani la watu? Kama unaipenda nchi yako mbona huungi mkono chochote cha kitanzania kiwe ni sanaa au bidhaa za nyumbani?
Maswali yanayohoji “uzalendo” wetu ni mengi kupita kiasi. Ninaposema hatuipendi nchi yetu huwa najaribu kuangalia jinsi gani wengi wetu tunaishi katika “uzalendo” kwa kufanya hasi ya mambo niliyoyataja hapo juu ambayo ni machache tu. Je “uzalendo” wetu ni ushabiki tu usio na maana yoyote? Tunaposema tunaipenda nchi yetu huwa tunamaanisha nini?
Nyerere aliturithisha rushwa? Nyerere aliturithisha uzembe na uvivu, kutowajibika? Hiyo ndio misingi ya taifa letu? Ni wazi kabisa kwamba Hayati Mwalimu Nyerere alijitahidi sana kuhakikisha kwamba uzalendo kwa nchi yetu unakwenda na vitendo. Kama alifanikiwa au alifeli pia jibu lipo miongoni mwetu sisi wenyewe,kila mmoja wetu. Tafakari.
Nimefikia kuandika juu ya “uzalendo” tena kwa sababu naamini huo ndio msingi wa kujenga nchi. Hizi nchi za wenzetu zimejengwa kwa kutumia msingi wa uzalendo. Ukiwa hapa Canada au Marekani unaona kabisa jinsi gani wenzetu wanazipenda nchi zao.Utathibitisha hilo kwa kuangalia jinsi ambavyo wanajitolea pindi wanapohitajika.
Wanaamini kwamba nchi ni yao na wao ndio wa kuijenga au kuibomoa,chaguo ni lao. Kwa bahati mbaya kwetu sisi tunadhani kuwa “mzalendo” ni pale tu unapotamka kwamba unaipenda nchi yako huku vitendo vyako vikithibitisha chuki mbaya uliyonayo.
Najua wengi mtasema “ah Jeff,sisi tunaipenda nchi yetu sana tu,tatizo ni viongozi wetu ndio wanatuangusha” Nitakuuliza,unadhani hizi nchi zilizoendelea huwa zinaongozwa na malaika? Jibu ni hapana,zinaongozwa na watu,tena wengi wao ni wala rushwa kama wetu tu, tofauti ni kwamba wananchi wanatambua kwamba uzalendo ni pamoja na kuhakikisha tunachagua viongozi na sio watawala.
Na isitoshe wanaamini kwamba kiongozi akikosea basi hana budi kuondolewa.Hakuna kulindana kwa sababu kama unamlinda kiongozi mbovu,basi hata wewe huna mapenzi kwa nchi yako. Nchi ni watu na sio viongozi peke yao.
Kwa kumalizia naomba ndugu msomaji,baada ya kumaliza kusoma hii makala,jiulize nini unaifanyia nchi yako ili kuthibitisha “uzalendo” wako? Tuipende nchi yetu kwa vitendo na sio maneno.
jeffmsangi@sympatico.ca
www.harakati.blogspot.com