WAKAZI wa Mbezi Luis Mshikamano, Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, wamekumbwa na hofu kutokana na kukithiri kwa matukio ya uhalifu.
Baadhi ya wakazi hao waliozungumza na Tanzania Daima, hivi karibuni, walisema mfululizo wa vitendo vya uhalifu, kujeruhiwa na kuporwa mali kunawafanya waishi kwa hofu.
Wiki iliyopita, walifanya mkutano wa kuweka mikakati ya kujilinda na baadaye walifanya maandamano hadi kituo cha polisi cha Mbezi ili kufikisha kilio kwa askari wa kituo hicho.
Mwenyekiti wa kikao hicho, Rymos Maruchu, alisema kutokana na hali mbaya ya kiusalama, wananchi wanapaswa kujipanga kujilinda wenyewe.
Alisema iwapo watajitolea kuendesha ulinzi na jeshi la polisi kushirikiana na wananchi hali hiyo inaweza kubadilika.
“Wote mnakumbuka tukio la kutisha la hivi karibuni la kuuawa kwa Gines Silayo (32) kutokana na kipigo alichokipata kutoka kwa majambazi akiwa na jirani zake wanne.
“Walivamiwa na majambazi wakiwa kwenye baa ya Nova iliyopo eneo hili na kujeruhiwa kwa kupigwa nondo, wakaporwa pesa ndogo za matumizi walizokuwa nazo na simu za mkononi.
“Ili tuepukane na matukio kama haya, ni lazima tuanze kujilinda wenyewe,” alisema Maruchu.
Alisema katika kipindi cha miezi mitano, baa tatu zimevamiwa na wateja kuporwa mali na kujeruhiwa kwa vipigo, na kwamba matukio hayo yanatokea kati ya saa mbili na saa tatu na nusu usiku.
Reginald Msengi, ambaye alikuwa katibu wa kikao hicho alisema kuwa, maeneo hayo yamepanuka kutokana na ujenzi, hivyo ili kuimarisha ulinzi kwenye eneo hilo wananchi wenyewe wanatakiwa kujitolea.