WAZIRI Mkuu, Edward Lowassa anakaimu nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kazi hiyo ameianza jana baada ya Rais Jakaya Kikwete kuanza ziara ndefu kwenye nchi za China, Japan, Korea Kusini na Falme za Kiarabu (UAE).
Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohammed Shein, nae ameondoka nchini jana kuelekea mjini Roma, Italia, kwa ziara ya siku tisa kuhudhuria kikao cha 32 cha Kamati ya Hifadhi ya Chakula, anakomwakilisha Rais Kikwete.
Rais Kikwete atakuwa na mazungumzo na wakuu wa nchi hizo na anatarajia kuanza ziara yake nchini Japan kwa ajili ya kuishirikisha nchi hiyo katika mambo ya miundombinu.
Katika ziara yake, Rais Kikwete ameambatana na mkewe, mama Salma Kikwete; Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji, Dk. Juma Ngasongwa; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Serikali ya Mapinduzi Zanzibar anayehusika na fedha na uchumi Dk. Mwinihaji Makame; Naibu Waziri wa Fedha, Mustafa Mkullo na Mbunge wa Muhambwe, Felix Kijiko (CCM).