Na Daniel Mjema,Moshi
WAKATI Serikali ikikabiliwa na tishio la kuporomoka kwa uchumi kutokana na mgawo wa umeme, msanii maarufu nchini, Omari Mwariko, ameibuka na kumwomba Rais Jakaya Kikwete kuingilia kati ili aweze kulipwa fidia ya mabilioni ya shilingi anayoidai Jeshi la Polisi..
Msanii huyo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Nyumba ya Sanaa ya Mwariko’s Art Gallery ya mjini Moshi amedai kuwa, anadai fidia ya mabilioni ya fedha kutokana na lori la kikundi hicho, kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro tangu mwaka 1983 na gharama za usumbufu ambao ameupata katika kipindi hicho.
Katika barua yake aliyoandika hivi karibuni yenye kumbukumbu MAG/KILIO/VOL.2006 kwenda kwa Rais Kikwete, Mwariko anadai kiasi hicho cha fedha baada ya Mahakama ya Uhujumu Uchumi kutupilia mbali kesi dhidi yao mwaka 1984 na kuamuru arudishiwe lori na mali zote zilizokuwamo ambazo alidaiwa kuzipata kwa njia isiyohalali.
Anadai pamoja na mahakama hiyo kuamuru warudishiwe lori hilo aina ya Bedford lenye namba za usajili MS 8345, bado polisi mkoani humo, wanaendelea kulishikilia bila uhalali huku baadhi ya vipuri vyake vikiwa vimeibwa.
Mwariko aliyemtengenezea kifimbo Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere , alidai lori hilo kabla ya kushikiliwa na polisi lilikuwa chini ya mkataba wa kulikodisha kwa Sh 40,000 kwa mwezi na kwamba kutokana na hatua hiyo ya polisi, walivunja mkataba, hivyo anahitaji fedha za kumlipa mteja wao. Athari nyingine ambazo anadai amezipata kutokana na kuzuiliwa kwa gari hilo ni kufilisika kwa biashara yake na kupoteza hadhi katika jamii.
Nakala ya barua hiyo ya Mwariko kwenda kwa Kikwete imetumwa kwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, Katibu Mkuu Wizara ya Usalama wa Raia, Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo na Katibu Mkuu Baraza la Sanaa la Taifa.
Nyaraka ambazo Mwananchi ina nakala zake, zinaonyesha kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais, iliwahi kuingilia kati suala hilo, mwaka 1989 na kuamuru lori hilo lirudishwe kwa mmiliki wake.
“ Waziri wa Mambo ya Ndani aliagiza Inspekta Jenerali wa polisi anunue vipuri vilivyoibwa katika gari lililotajwa likiwa chini ya ulinzi wa polisi kituo cha mkuu Rombo ili mhusika arudishiwe gari lake,” inasomeka sehemu ya moja ya nyaraka hizo.
Barua hiyo ya Septemba 18,1989 yenye kumbukumbu PMC/DSM/C.230/16 ilidai kuwa, hadi tarehe hiyo, IGP alikuwa hajachukua hatua yoyote ya kulifufua gari hilo ingawa alikuwa ameahidi kufanya hivyo.
Kutokana na kutotekelezwa kwa maagizo ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais, alidai ofisi hiyo ilimuandikia barua Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro ikionyesha kusikitishwa na hatua hiyo.
Barua ya Septemba 26, mwaka1990 yenye kumbukumbu P.70/6/X1/126 inasomeka” linalotatiza na kushangaza ni kwamba msururu huo wa barua na maagizo kwamba Mwarikos atengenezewe gari lake na arejeshewe haraka haijatekelezwa.
Hata hivyo, katika hali inayoonyesha angalau Polisi Mkoa Kilimanjaro imeanza kulifanyia kazi suala hilo, Ijumaa iliyopita Kamanda wake, Venance Tossi alimwita Mwarikos na kumtaka achukue lori lake.
“ Nimeshamiwita na nimeshampa barua ya kumtaka achukue lori lake mara moja kwa sababu suala la yeye kufidiwa serikali ilishalikataa kwa hiyo mweleze na wewe kwamba aje achukue lori lake,” alisema Kamanda Tossi.
Mwarikos alipohojiwa jana, alishikilia msimamo wa kutaka alipwe fidia kwa sababu polisi waliendelea kulishikilia lori hilo kwa miaka hiyo 20 bila kosa lolote licha ya mahakama kuamuru liachiliwe.
“ Wananipaje bila fidia hili lori kama lingekuwa limeendelea kufanya kazi hivi sasa ungekuta tulishanunua lori la kisasa, lakini wamekaa nalo, limepitwa na wakati, limeibwa vipuri halafu wanatuambia njoo mchukue lori lenu, ” alilalamika