Na Ramadhan Semtawa
MWAFRIKA wa kwanza kuongoza Idhaa ya Kiswahili ya Radio ya Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), Danstan Tido Mhando, ambaye ni Mtanzania amestaafu kazi na anategemea kurejea nchini hivi karibuni.
Tido alitangaza uamuzi wake wa kustaafu rasmi jana huku taarifa zikieleza kwamba huenda akapewa uongozi wa moja ya nafasi nyeti za mawasiliano nchini.
Tido ambaye aliondoka nchini akiwa mtangazaji kabla ya kujiunga na BBC alitokea KBC ya Kenya katika miaka ya 1980. Alianza kazi ya Ukuu wa Idhaa ya Kiswahili mwaka 1999. Aliwahi kufanya kazi Radio Tanzania Dar es Salaam ( RTD).
Akizungumza katika Kipindi cha Wiki Hii jana ambacho amekuwa akikiendesha, Tido alisema kikubwa kilichomfikisha katika nafasi hiyo ni kujiamini na kujituma.
Alifafanua kwamba, wakati mwingine waandishi wa vyombo vingine wamekuwa wakihoji vipi amekuwa na uwezo wa kuzungumza na Marais katika maeneo ambayo ni magumu kwao kuweza kufanya hivyo.
Alisema kikubwa alichojifunza pia katika hilo la kuwahoji hata Marais ni kwamba wao wanataka kuheshimiwa na pia wanaangalia uwezo wa mwandishi katika kuuliza.
Kuhusu mafanikio katika uongozi wake, alisema moja ya mafanikio ambayo ni kutokana pia na ushirikiano wa timu nzima ya BBC, ni pamoja na kufungua ofisi katika kila kituo kikuu katika nchi mbalimbali na kuongeza teknolojia katika urushaji matangazo.
Alitaja mafanikio hayo ya teknolojia kwamba ni pamoja na kuwezesha wasikilizaji wa BBC kuweza kupata matangazao hayo moja kwa moja kwa kutumia Intaneti.
Tido alisema angeweza kuendelea na mkataba wa miaka saba zaidi lakini ameamua kustaafu ili kurudi nyumbani Tanzania kutoa mchango wake katika kuendeleza sekta ya habari.
Mtangazaji huyo amejipatia umaarufu mkubwa kutokana na uwezo wake wa kuuliza maswali magumu kwa wale anaowafanyia mahojiano wakiwemo Marais.