.Wadai mishahara wamependelewa wenye taaluma tu
.Watishia kuandamana kwa Rais
Na Mwandishi Wetu
WAFANYAKAZI waendeshaji wa vyuo vikuu vya serikali nchini wamesema iwapo malalamiko yao kuhusu mishahara yatakuwa hayajashughulikiwa hadi Novemba, mwaka huu, wataandamana kwenda kumwona Rais Jakaya Kikwete.
Wamesema lengo litakuwa kumweleza kilio chao juu ya ukiukwaji wa mapendekezo ya kamati iliyoundwa na Rais kushughulikia mishahara yao, ambapo utekelezaji umewahusu wanataaluma tu na kuwaengua wafanyakazi waendeshaji.
Hayo yamo kwenye tamko la maazimio waliyofikia wafanyakazi hao, na kueleza kwamba hatua hiyo inatumika kama silaha ya mwisho. Kundi hilo linajumuisha pia vyuo vikuu vishiriki.
Tamko hilo, lililotolewa jana na Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Elimu ya Juu, Sayansi, Teknolojia na Utafiti (RAAWU), Adelgunda Mgaya, linasema Kamati ya Rais iliyoundwa Septemba mwaka jana, ilishauri tofauti ya mishahara ipunguzwe kwa uwiano kati ya asilimia 12 na 17.2, lakini watekelezaji wamekiuka agizo.
Kamati pia ilishauri nyongeza ya asilimia 100 kwa wanataaluma, kitu ambacho tamko linaeleza kimetekelezwa, lakini kwa wafanyakazi waendeshaji hakuna kilichotekelezwa kabisa.
“Hatua ya serikali kuboresha mishahara ya wahadhiri pekee na kuwaacha waendeshaji kinyume na maamuzi ya Kamati ya Rais, inachochea chuki na mgawanyiko wa watumishi kwenye vyuo vikuu na vyuo vikuu vishiriki vya umma,” ilisema taarifa hiyo.
Waraka huo wa wafanyakazi waendeshaji, unaonyesha kuwa utekelezaji umefanya uwiano kuwa wenye tofauti kubwa sasa hivi, yaani kati ya asilimia 59.7 na 80.7.
Wafanyakazi hao wa vyuo vikuu vya umma wanadai kwamba walishapita ngazi mbalimbali kutoa malalamiko yao, ikiwa ni pamoja na kuwasiliana na makatibu wakuu wa Wizara ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Msajili wa Hazina na Katibu Mkuu Kiongozi.
“Ufuatiliaji huo haukusaidia kupata suluhisho la tatizo, mbali ya kauli ‘Wafanyakazi waendeshaji hawahusiki na maamuzi ya Kamati ya Rais’. Kauli hizi zilitia shaka kwani taarifa ya Kamati ya Rais kwa Serikali, imeweka bayana maamuzi ya kuboresha mishahara ya watumishi waendeshaji,” linasema tamko.