Na Maura Mwingira, Arusha
MKE wa Rais Mama Salma Kikwete, amewataka watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu, kuweka juhudi katika masomo ili wajipatie uhakika wa maisha mazuri hapo baadaye.
Mama Salma alitoa wito huo katika hafla ya chakula cha mchana alichokiandaa maalum, kwa ajili ya watoto yatima, ambao alikula nao katika Ikulu ya Arusha, kusherehekea sikukuu ya Idd el Fitr.
“Ombi langu kubwa kwenu ni hili, zingatieni elimu, nawaomba sana usikimbie shule jitahidini kwa bidii zote, someni ili baadaye elimu iwasaidia ninyi wenyewe na jamii, hili ndio ombi langu kubwa kwenu,” aliwasihi watoto hao.
Aliwaambia watoto hao kutoka katika vituo mbalimbali vya kulelea yatima katika mkoa wa Arusha, kwamba elimu ndio mkombozi wao wa pekee, na kwamba bila kuzingatia elimu hawatakuwa na maisha bora.
Pamoja na kuwasisitizia watoto hao, umuhimu wa kuzingatia elimu, Mama Salma pia ameikumbusha jamii ya Watanzania kwamba jukumu la kuwalea watoto yatima na wale wanaoishi katika mazingira magumu si la serikali peke yake, bali ni la Watanzania wote.
“Watoto yatima si wa serikali, kila mtu pale alipo anawajibika kuwasaidia kwa hali na mali watoto hawa, tunapaswa kuwalea na kuwatunza kama tunavyowalea watoto wetu majumbani mwetu,” alisisitiza.
Alisema jamii inawajibika kuwapatia watoto hao malezi mema na maadili yanayofaa katika ukuaji wao kwa kuwa watoto hao ni wajamii.
Pamoja na kula nao chakula cha mchana, Mama Salma alitoa zawadi mbalimbali kwa watoto hao.
Wakizungumza kwa niaba ya watoto wenzao, Emmanuel Zadok na Janet John, walisema hatua hiyo ya Mama Salma kula nao chakula katika sikukuu hiyo muhimu ni jambo ambalo halitawatoka katika mioyo yao.
Walisema wamefarijika sana kwa moyo wake wa upendo, huruma na imani aliyoionyesha kiasi cha kutenga muda wake na kula nao katika sikukuu ya Idd el Fitr.
Walimuahidi kwamba wataongeza bidii katika masomo yao kwa kuwa wanatambua elimu ndio mkombozi wao.
Awali, Kaimu Ofisa Ustawi wa Jamii, Mkoa wa Arusha, Asha Mohammed, pamoja na kumshukuru Mama Salma kwa moyo wake wa upendo kwa watoto hao, alishauri kwamba ifike mahali jamii ya Watanzania ijenge utamaduni wa kuwasalimia watoto hao na kuwalea kama watoto wao.