Na Peter Katulanda, Musoma
RAIS Jakaya Kikwete amewataka viongozi hususan wakuu wa mikoa kuwa wabunifu ili rasilimali zilizopo mikoani zitumike kuleta maendeleo na kuondoa umaskini kwa wananchi.
Alitoa wito huo jana wakati wa ufunguzi wa mkutano wa wawekezaji wa Mkoa wa Mara, uliofanyika mjini hapa katika ukumbi wa wawekezaji wa mkoa.
Rais Kikwete alisema moja ya udhaifu ambao umekwamisha wawekezaji kuja nchini ni kutotangaza kikamilifu rasilimali zilizopo nchini, hali iliyofanya watu kuijua Dar es Salaam pekee kuwa ndipo mahali pa kuwekeza.
Alisema kukwama kuzitangaza rasilimali hizo, kumetokana na baadhi ya viongozi wa ngazi za mikoa kutojua fursa zilizomo katika maeneo yao
kutokana na kukosa ubunifu, kuendekeza ratiba za kupangiwa kutembelea miradi na maeneo badala ya wao kupanga cha kufanya.Akizungumzia Mkoa wa Mara, alisema ni mkoa ambao una rasilimali nyingi lakini kutokana na kutofahamika na kutotangazwa umekuwa nyuma kimapato.Rais Kikwete amempongeza mkuu wa mkoa huo, Isidori Shirima kwa kuanzisha utaratibu wa kuzitangaza rasilimali zilizopo."Nakupongeza kwa kuwa kiongozi mbunifu na mwenye mawazo mapya ya kuleta maendeleo. Natambua ulipokuwa Mtwara miaka michache iliyopita, uliandaa mkutano kama huu na sasa baada ya kukaa hapa kwa kipindi kifupi kisichozidi mwaka mmoja, umewezesha kufanyika kwa mkutano huu," alisema Kikwete.Alisema takwimu zinaonyesha Mara umekuwa wa sita kwa kuwa na ng'ombe wengi nchini, lakini utajiri huo mkubwa bado hauleti tija kwa wananchi na kuwafanya wafugaji kuwa watumwa wa ng'ombe badala ya ng'ombe kuwa watumwa wao hali aliyosema inapaswa kubadilika.Rais Kikwete alisema wafugaji wamekuwa wakifuga mifugo mingi wakidhani ndiyo utajiri na kujivunia k
uwa na ng’ombe wengi huku wakilala mahali pabaya, kutokula vizuri na kutosomesha watoto wao.
Alisema mwaka 1995 na 2000 Mkoa wa Mara ulichangia pato la taifa kwa wastani wa asilimia 3.45 kwa mwaka na kuwa mkoa wa 13 kati ya mikoa yote nchini.
Rais Kikwete alisema mchango huo, ulikuwa ni mdogo ikilinganishwa na Mkoa wa Shinyanga ambao ulifikia asiliamia 8.09 na kuchukua nafasi ya pili kitaifa licha ya kuwa rasilimali zinazofanana na za mkoa huu.
Alisema changamoto katika kuvutia wawekezaji ni kufufua miradi ya umwangiliaji na kuweka miundombinu bora kama barabara za lami na kuboresha uwanja wa ndege kuwa wa kiwango cha lami.
Kwa upande wa uvuvi, alisema bado wanaweza kuongeza uwekezaji kwa kuendelea kujenga viwanda vya kusindika minofu ya samaki na kusaidia wachimbaji wadogo ili waweze kuwezeshwa.
Akizungumzia madini, Rais Kikwete alisema mkoa una nafasi ya kujenga kiwanda cha saruji kutokana na kuwa na madini ya chokaa hasa ikizingatiwa viwanda vilivyopo nchini havikidhi soko la ndani na nje.
"Nilikuwa Afrika Kusini nikakuta wanahitaji tani 100,000 za saruji nikasema hiyo kwetu tunaweza kuja hapa nikaeleza wenye viwanda vyetu wakajitahidi ikashindikana sasa tunaweza kulitazama eneo hili kutokana na kuwa na madini ya chokaa kwani soko la uhakika lipo,” alisema Kikwete.
Alisema juhudi za kuanzishwa kwa mkutano huu wa wawekezaji kuutangaza Mkoa wa Mara zitaungwa mkono na serikali na kusaidia pale watakapo hitaji msaada wa kitaifa.