.Ataka maslahi ya taifa yawekwe mbele, si uroho wa madaraka
.Ashutumu wenye kudekeza malumbano
Na Khatib Suleiman, Zanzibar
KATIBU Mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad, amewataka wafuasi wake kutulia huku wakimsubiri Rais Jakaya Kikwete kuendelea kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa kisiasa Zanzibar.
Alisema ni vyema kwa wanachama wa CUF kuwa watulivu katika kipindi chote hiki, huku Rais Kikwete akishughulikia na kuupatia ufumbuzi mgogoro wa kisiasa wa visiwa vya Unguja na Pemba.
Akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake Mtoni, nje kidogo ya mji wa Zanzibar, Seif alisema Rais Kikwete ameonyesha nia nzuri ya kuupatia ufumbuzi mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar hivyo wananchi hawana budi kumpa nafasi.
“Acheni tumpe nafasi Rais Kikwete kufanya kazi ya kuupatia ufumbuzi mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar, kazi ambayo anaifanya kwa sasa. Hata ziara yake ya hivi karibuni visiwani hapa ni ushahidi tosha,” alisema Seif.
Hata hivyo, alisikitishwa na kauli za baadhi ya wanasiasa ambao kwa makusudi wamekuwa wakivunja moyo juhudi za Rais Kikwete katika kuupatia ufumbuzi mgogoro wa kisiasa, ikiwemo kuanzisha lugha za malumbano.
Alisema huu si wakati wa kuanzisha malumbano katika siasa, “hasa katika suala hili ambalo linagusa hisia za wananchi wengi pamoja na maslahi yao ya baadaye” na akawataka viongozi wa kisiasa siku zote kuweka mbele maslahi ya umma.
“Nawataka viongozi wenzangu wa kisiasa kuweka mbele maslahi ya kitaifa kuliko ubinafsi wa madaraka kwani sisi ni viongozi wa wananchi na iko siku tutaulizwa na wananchi wenyewe,” alisema Katibu Mkuu wa CUF.
Aliyataja baadhi ya mapendekezo ya CUF ambayo Rais Kikwete ameahidi kuyapatia ufumbuzi, ikiwemo kuundwa kwa serikali ya mseto ambayo itaunganisha nguvu za vyama vyote viwili vya siasa - CCM na CUF.
Seif alisema chama cha CUF hakina matatizo na kuwepo suala la serikali ya mseto, jambo ambalo alieleza kuwa yeye binafsi alikuwa akilipigia kelele siku zote tangu kipindi cha kampeni katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana.