MTOTO Mohamed Salehe, mwenye umri wa kati ya miezi sita na saba, aliyepotea kwao Mpwapwa katika mazingira ya kutatanisha, ameokotwa akiwa hai kando ya barabara ya Kijiji cha Mvumi Makulu akiwa hai.
Mtoto huyo ambaye alipotea Ijumaa ya Oktoba 13 mwaka huu, amekutwa kando ya barabara hiyo akiwa ameshikishwa chupa ya chai ikiwa imejaa maziwa huku akiwa amevishwa vizuri.
Kwa mujibu wa mama mzazi wa mtoto huyo aliyejulikana kwa jina moja tu la Angela, anasema mtoto huyo aliokotwa Oktoba 15 majira ya saa nne asubuhi, na wachungaji wa kanisa moja la Anglikana kijijini hapo.
Amesema kuwa wachungaji hao walipata taarifa kwa watoto wadogo ambao waliliona gari moja dogo (teksi) iliyofika katika eneo hilo na watu wawili wote wanawake kushuka na kumtupa mtoto huyo kisha kutoweka.
Amesema watoto hao walipoona kuwa kuna kitu kimetupwa walikwenda kuangalia na kushangaa walipoona ni mtoto mwenzao akiwa ameshikilia chupa ya chai.
Mama huyo alisema watoto hao walikwenda kanisani kutoa taarifa ya ya kumwona mtoto huyo ndipo wazee wa kanisa walipokwenda kwenye eneo hilo, walimkuta mtoto huyo na kutoa taarifa kwenye kituo cha polisi.
Mtoto huyo alipelekwa hospitali kupimwa afya yake na alikutwa hana tatizo lolote na wazee hao walimwacha hospitali hapo na kumlipia matibabu.
Amesema kuwa siku ambayo mtoto huyo aliibwa alikuwa shuleni na alimwacha mtoto na bibi yake ambaye pia alitoka kwenda kutafuta kuni na kumwacha mtoto peke yake nyumbani.
Amesema kuwa bibi huyo aliporudi hakumkuta mtoto na ndipo alipoenda polisi kutoa taarifa kupotea kwa mtoto huyo.
Mama huyo alisema baada ya majirani zake kupata taarifa ya kupote kwa mtoto huyo walianza kuwasaka wasichana wawili, Asha Ndobwe na Asha Malingo, ambao walisemekana kutafuta watoto kwa muda mrefu bila mafanikio.
Wasichana hao waliohisiwa kuiba mtoto huyo walikimbilia Kongwa kabla ya kutorokea Dodoma, baada kugunduliwa na ndugu waliokuwa kwao kuwa wanakaa na mtoto asiyekuwa wao.
Walipofika Dodoma mjini walihisi kama vile watakamatwa ndipo waliamua kumtupa nje kidogo ya Manispaa ya Dodoma.
Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho, Paschal Mangwelah amethibitisha kuwapo kwa tukio hilo na kusema kuwa wameamua kumpa mama huyo mtoto huyo baada ya kuthibitisha kuwa ni wake.