TAASISI ya dini ya Good News For All Ministry kwa kushirikiana na madhehebu 43 leo itakuwa na mkesha wa kitaifa kuliombea taifa na bei ya mafuta katika soko la dunia ishuke.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Askofu Charles Gadi, mkesha huo utafanyika kwenye viwanja vya Jangwani, jijini Dar es Salaam.
Askofu Gadi katika taarifa yake alisema katika mkesha huo wataombea kumalizika kwa mgogoro Mashariki ya Kati, kati ya Israel na Palestina, Irak na mgogoro unaofukuta kati ya Iran na Marekani.
Alisema migogoro hiyo imekuwa ni sababu ya kupanda bei ya mafuta katika soko la dunia na kupanda gharama za maisha katika nchi kadhaa ikiwemo Tanzania.
Bei ya mafuta katika soko la dunia hivi sasa imepanda na kufikia dola za Marekani 75 kwa pipa moja (zaidi ya sh. 75,000 za Tanzania).
Nchini Tanzania bei ya petroli imepanda toka sh. 800 kwa lita moja ambapo hivi sasa imepanda hadi kufikia sh. 1,400 kwa lita moja ya petroli na dizeli sh. 1,200.
Upande wa bei ya mafuta pia umesababisha kupanda kwa gharama za maisha, ikiwemo nauli za mabasi na bidhaa mbalimbali nchini.
Askofu huyo alisema iwapo migogoro hiyo itakwisha hali ya maisha huenda ikawa nafuu. Pia, alisema wataombea bajeti ya mwaka huu ya serikali ichambuliwe na kupangwa na bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kulingana na mahitaji na matarajio ya Watanzania.
Alisema pia wataomba Mungu waondolee Watanzania roho chafu iliyozuka hivi karibuni ya kuiba watoto na kuwateka kwa lengo la kujipatia fedha.
Mkesha huu wa kitaifa utakaofanyika Jangwani leo ni utaratibu wa kila mwisho wa mwezi wa shirika hilo uliojiwekea kwa kushirikiana na madhehebu 43 kuliombea taifa katika mambo mbalimbali ya kijamii, kiuchumi na kisiasa yafanyike kama Mungu anavyotaka.
Kutoka gazeti la Uhuru
ISSN 0876-3896 NA.19321
Na Mwandishi Wetu