WIZARA ya Usalama wa Raia imesema kuwa, itaongeza idadi ya askari wa usalama barabarani jijini Dar es Salaam na miji mingine mikubwa yenye msongamano wa magari, ili kusaidia kazi ya kuyaongoza magari hayo kwa kubadilishana, kwa lengo la kupunguza msongamano.
Waziri wa wizara hiyo, Bakari Mwapachu alisema hayo jana baada ya kumaliza ziara ya ghafla ya kuzungukia maeneo yote yenye msongamano mkubwa wa magari barabarani aliyoifanya kwa helikopta.
Katika ziara hiyo iliyoanza saa 1:00 alfajiri hadi saa 3:00 asubuhi jana, Waziri Mwapachu alifuatana na Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Saidi Mwema, Kamishna wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Alfred Tibaigana na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Polisi cha Dar es Salaam, Elice Mapunda.
Alisema kuwa doria hiyo ya helikopta itawezesha kuishauri serikali juu ya kupunguza tatizo la msongamamo na hata kutunga sheria na kuzifanyia marekebisho sheria zilizopo zihusuzo usalama barabarani.
Alisema kuwa, ujumbe wake umebaini kuwa tatizo kubwa la msongamano wa magari jijini Dar es Salaam, unasababishwa na matumizi mabaya ya barabara unaofanywa na madereva, wakiwamo wa mabasi ya daladala kupenyeza pembeni na mengine kusimama ovyo kwa kupakia ama kuteremsha abiria na miundombinu duni.
Ziara hiyo pia imebaini kuwa, barabara nyingi zimejengwa bila ya kuwekwa vituo vya kupakia na kuteremsha abiria, jambo ambalo linawalazimu madereva kukiuka sheria kwa kusimama ovyo katika maeneo yenye abiria kwa kupakia na kuteremsha.
Mwapachu pia alitumia fursa hiyo kuwaomba wadau na wananchi mbalimbali kuendelea kulisaidia Jeshi la Polisi kwa kuwapatia askari vyombo vya mawasiliano yakiwamo magari, pikipiki na redio call kwa lengo la kusaidia katika mapambano dhidi ya uhalifu.
Alisema kuwa baada ya kazi kubwa ya kupambana na majambazi na hali kuonyesha kufanikiwa, jeshi hilo sasa limeingia katika hatua nyingine ya kupambana na msongamano wa magari na ajali za barabarani.
IGP Mwema, akizungumza kwenye mkutano huo uliofanyika ofisini kwa Waziri Mwapachu, aliwaomba wananchi kuendelea kutoa taarifa mbalimbali zitakazoliwesha jeshi hilo kuendelea na mapambano dhidi ya wahalifu, wakiwamo wale wanaovunja kanuni na sheria za usalama barabarani