MKAZI wa Kijiji cha Somanda, Kata ya Mpindo, Masele Maduhu (35), ameuawa kwa kupigwa na wananchi baada ya kuwavamia na kuwajeruhi kwa mapanga wanawake wawili.
Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Shinyanga, Siro Nyakoro, alisema jana kuwa katika shambulio hilo wanawake hao, Tabu Mboje (28) na Mtugwa Phares (32), wakazi wa Mbalagane walijeruhiwa sehemu mbalimbali mwilini na wamelazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa. Hali zao zinaendelea vizuri.
“Kutokana na kelele za kuomba msaada za wanawake hao, wananchi wenye hasira walijitokeza na kumshambulia Maduhu kwa kipigo cha ngumi, mateke, marungu na fimbo hadi kusababisha kifo chake,” alisema Kamanda Siro.
Katika tukio jingine, wanawake wawili wameaua kikatili kwa kukatwa mapanga baada ya kuvamiwa walipokuwa wamelala.
Wanawake waliouawa wametajwa kuwa ni Moligu Nzagamba (38) na Nuja Lugambija (50).
Akielezea tukio hilo, Kamanda Siro alisema, wanawake hao walifikwa na mkasa huo baada ya kwenda kwa mganga wa jadi, Korokoro Gwalugwa, katika Kijiji cha Gambusi kwa lengo la kutafuta tiba kutokana na matatizo yanayowakabili.
“Baada ya kuonana na mganga na kumweleza shida yao waliambiwa walale mahali hapo kwa ajili ya matibabu au uchunguzi zaidi na ndipo walipovamiwa na kushambuliwa kwa kukatwa kwa mapanga na kusababisha vifo vyao,” alisema.
Kutokana na mauaji hayo, mganga huyo ametoroka na polisi wanaendelea kumsaka na kwamba watu wengine watatu; Kija Hela (50), mkazi wa Kijiji cha Gambusi, Emma Phares (46), mkazi wa Kibara, Bunda mkoani Mara na Kisherya Mgayambogo (40), wanashikiliwa kwa tuhuma za mauaji hayo.