WAKAZI wa Mabibo, Kata ya Jitegemee, Dar es Salaam wameulalamikia uongozi wa kata hiyo kwa kushindwa kuwaondoa watu waliovamia ardhi katika eneo hilo na kuyang’oa mabomba ya umma.
Wakizungumza na Tanzania Daima kwa nyakati tofauti, baadhi ya wakazi hao wameeleza kuwa katika maeneo hayo kulikuwa na mabomba ya umma ambayo yalijengwa enzi ya Serikali ya Awamu ya Kwanza.
Wakazi hao walieleza kuwa wanaamini watu hao wamepata maeneo hayo kutokana na mazingira ya rushwa.
“Inawezekana baadhi ya viongozi wa kata hiyo walihongwa na watu hao na kuwaachia kujenga sehemu hizo kinyume cha utaratibu.
“Ni rushwa tu, hakuna jingine, kwa sababu haya mabomba yalijengwa kipindi cha Braiton alipokuwa mbunge wa jimbo hili (Ubungo) na wananchi tuliyatumia kwa kuchota maji, sasa leo hii watu wamehodhi sehemu hizo kwa kubomoa mabomba hayo na kujenga maduka na sehemu za kuishi, na uongozi umeona na umeamua kukaa kimya.
“Sasa kwa nini tusihisi kwamba wamekula rushwa? ” alisema mmoja wa wakazi hao.
Akizungumza kwa njia ya simu juzi, Diwani wa kata hiyo, Kassim Lema, alipoulizwa kuhusu suala hilo alikiri kuwapo kwa watu waliovamia maeneo hayo na kujenga maduka na makazi ya kuishi.
Lema alisema baada ya kutokea suala hilo aliwasiliana na watendaji wa kata hiyo ili wavamizi hao waondolewe, lakini kunaonekana kuna ugumu kwa watendaji katika kutoa maamuzi.
Kutokana na hali hiyo, diwani huyo aliitaka Tanzania Daima kuwasiliana na Mwenyikiti wa Serikali ya Mtaa wa kata hiyo, kwani suala hilo muda mrefu lilishawasilishwa kwenye ofisi yake.
Akizungumzia suala hilo, mwenyekiti huyo, Omari Chikoyo, alikiri kuwapo kwa tukio hilo na akasema wao kama viongozi waliwafuatilia wavamizi hao na kuwataka wabomoe maduka na nyumba hizo, lakini walikataa kwa kudai ni maeneo wanayoyamiliki kihalali.
Alisema baada ya watu hao kukaidi amri hiyo hivi sasa wana mpango wa kwenda katika ngazi za juu za uongozi wa serikali, ili kupatiwa msaada, watu hao waondoke