MAOFISA wa ulinzi wa Uingereza, wamesema nchi yao kwa sasa inawindwa zaidi na al- Qaeda, hasa baada ya shambulizi lililofanyika nchini humo, Julai 7, na kuua watu 52.
Maofisa hao wanasema hali imekuwa ya wasiwasi tangu kipindi hicho na kuwa ulinzi zaidi umewekwa kila mahali kuhakikisha kuwa mashambulizi zaidi hayatokei.
Wanaamini kuwa kwa sasa mtandao huo unaendeshwa kupitia vikundi vidogo vidogo vilivyoundwa ndani ya Uingereza, ambavyo vina silaha za maangamizi na kuwa mashambulizi ya Julai 7, yalikuwa ni mwanzo tu.
Vikundi hivyo kila kimoja kina kiongozi wake na vinashughulika na silaha za maangamizi, na vikundi hivyo vinafanya kazi katika maeneo tofauti na kuna kiongozi anayesimamia vikundi kadhaa kwa pamoja.
“Miaka mitano iliyopita ilikuwa ikifikiriwa kuwa al-Qaeda ni mtandao tu ambao haukuunganika, wenye lengo moja, lakini kwa sasa ni mtandao ambao umejipanga kwa namna ya ajabu,” anasema Crispin Black mchunguzi wa mambo ya usalama.
Wanausalama wana wasiwasi kuwa mtandao huo kwa sasa unajipanga kushambulia vyuo vikuu na taasisi nyingine za kijamii.
Hata hivyo, mchunguzi huyo amesema shambulizi lingine nchini humo kwa sasa sio rahisi kwa kuwa wanausalama wamejipanga vizuri.
Alisema wanausalama kwa sasa wanatambua ni nani wanayemtafuta na wamepewa mafunzo ya uhakika ya namna ya kupambana na wanamtandao hao.