RAIS Jakaya Kikwete amempunguzia madaraka, aliyekuwa Naibu Katibu wa Rais na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Ikulu, Balozi Peter Kallaghe.
Kwa mabadiliko hayo, Balozi Kallaghe sasa anabaki kuwa Mkurugenzi wa Mawasiliano.
Nafasi ya Naibu Katibu wa Rais sasa itashikwa na Chabaka Kilumanga.
Taarifa iliyotolewa na Ikulu, Dar es Salaam, jana ilisema uteuzi huo ulianza rasmi Oktoba 17, mwaka huu.
Kabla ya uteuzi huo, Kilumanga alikuwa Ofisa Mambo ya Nje Mkuu Daraja la Pili na Mkuu wa Utawala katika Ubalozi wa Tanzania Abu Dhabi.
Huu ni mwendelezo wa mabadiliko mbalimbali serikalini, yanayoendelea kufanywa na Rais Kikwete tangu ashike madaraka ya kuiongoza nchi Desemba, 2005.
Amekuwa akifanya mabadiliko taratibu, huku akiendelea kuwa na timu ya watumishi iliyokuwapo ama wakati wa uongozi wa Rais mstaafu, Benjamin Mkapa, au wakati wa Rais mstaafu, Ali Hassan Mwinyi.
Wiki hii alifanya mabadiliko kwa kuwahamisha mawaziri 10 na naibu mawaziri wanane. Hapakuwapo mabadiliko ya kuingiza au kumtoa nje ya Baraza la Mawaziri, waziri au naibu waziri yeyote.
Mabadiliko zaidi yanatarajiwa, kwani wakati akitangaza Baraza la Mawaziri Januari mwaka huu, alisema itakapobidi kufanya mabadiliko, watakaoguswa ni pamoja na viongozi katika ngazi nyingine