MSHITAKIWA Salum Masudi (30) anayekabiliwa na kesi ya mauaji, jana alifanya vurugu katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala kwa madai ya kutotendewa haki katika kesi hiyo.
Mshitakiwa huyo alifanya vurufu hizo baada ya Hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Mustafa Mlawa kuahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 30 kwa maelezo kuwa upelelezi wake haujakamilika.
Baada ya kutoka mahakamani, mshitakiwa huyo alipanda juu ya gari moja lililokuwapo mahakamani hapo huku akipiga kelele kuwa hatendewi haki, hivyo anataka kujinyonga.
Hali hiyo ilisababisha baadhi ya watu waliokuwapo mahakamani hapo kusubiri kesi zao kutajwa kutawanyika.
Kutokana na hali hiyo, askari waliokuwapo mahakamani hapo walimkamata na kumweka chini ya ulinzi, kisha akafunguliwa mashitaka ya kufanya fujo mahakamani.
Akisomewa mashitaka hayo na Mwendesha Mashitaka, Gervanus Muhume alidai kuwa jana, saa 4:00 asubuhi, alifanya vurugu katika mahakama hiyo, hivyo kusababisha kuvunjika kwa amani. Alikana tuhuma hizo na kesi itatajwa Oktoba 30