Japo Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini mtaafu, Omari Mahita ameagwa rasmi lakini ametoa ahadi inayotia matumaini pale aliposema ataendelea kuwa askari hadi mwisho wa maisha yake.
Mahita aliagwa jana na maofisa waandamizi wa Jeshi la Polisi huko mjini Moshi katika hafla ilihudhuriwa pia na mrithi wake IGP Said Mwema, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali George Waitara na Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa, JKT, Meja Jenerali Davis Mwamunyange.
Kwa upande wa Serikali, Naibu Waziri wa Usalama wa Raia Bw. Aboud Mohamed Aboud alimwakilisha Waziri wake, Bw. Harith Mwapachu katika hafla hiyo.
Katika hafla hiyo ambayo haikuwa na hotuba yoyote kutoka kwa viongozi hao, pia walikuwepo majaji kutoka Mahakama Kuu Kanda Kilimanjaro pamoja na wakuu wastaafu wa Jeshi hilo Samwel Pundugu na Haruni Mahundi.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Moshi baada ya hafla hiyo Bw. Mahita alisema licha ya kustaafu yeye bado ni askari na ataendelea kuwa askari mpaka atakapoingia kaburini.
Alisema yuko tayari kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi nchini kwa kuwashauri wakati wowote endapo watamtaka kufanya hivyo kwa madai kuwa yeye bado ni askari.
Pia Bw. Mahita aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa Jeshi hilo kwa kutoa taarifa za wahalifu hata kama ni ndugu zao kwani kinyume cha hapo matatizo hayataisha.
Bw.Mahita alistaafu mapema Machi mwaka huu baada ya kutimiza muda wake wa utumishi Serikalini ambapo alilitumikia Jeshi hilo kwa miaka 38, 10 akiwa IGP.
Bw. Mahita ambaye hivi sasa anajishughulisha na kilimo huko kwake mkoani Morogoro ni Inspekta Jenerali wa saba kushika wadhifa huo tangu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar April 26 1964.